April 27, 2021

WATAALAMU TANESCO KUENDELEA KUTEKELEZA MIRADI YA KIMKAKATI

 


Waziri wa Nishati, Dkt. Medard Kalemani akiwa katika kikao kazi na Watendaji wa TANESCO leo Aprili 25, 2021 Jijini Dodoma, amesema mradi wa njia kuu ya kusafirisha umeme kutoka Julius Nyerere hadi Chalinze kilometa 167 msongo wa kilovolti 400 utajengwa na Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO). 

Serikali imekuwa ikiwaamini na kuwatumia Wataalamu wa TANESCO katika kutekeleza na kusimamia miradi mbalimbali ya kimkakati ukiwemo wa Julius Nyerere utakaofua megawati 2115.

Dkt. Kalemani ameongeza kuwa njia hiyo ya umeme inatarajiwa kukamilika mwezi mmoja kabla ya mradi wa kufua umeme wa Julius Nyerere kuakamilika. 

Katika hatua nyingine Dkt. Kalemani amesema kuwa, Serikali imeridhishwa na utendaji kazi wa Wafanyakazi wa TANESCO na Wizara ya Nishati imekuwa ikijivunia utendaji kazi wao. 

"Ndugu zangu mafanikio ya nchi hii yanategemea TANESCO, vigezo vilivyofanya tuingie kwenye uchumi wa kati umeme umechangia kwa kiasi kikubwa sana" amesema Dkt. Kalemani. 

Maeneo ambayo TANESCO imekuwa na mafanikio ni eneo la kuunganisha Wateja ambapo TANESCO iliweka malengo ya kuunganisha Wateja 300,000 na kabla ya mwezi Juni mwaka huu wamesha unganishwa Wateja 322,000 hivyo kuvuka lengo.

Eneo lingine ni ukusanyaji wa madeni sugu ya Serikali na Taasisi za umma deni lilikuwa bilioni 278 ambapo zimekusanywa bilioni 126.

Dkt. Kalemani amesema katika bajeti ya mwaka ujao wa fedha wa 2020/21 Wizara imeainisha vipaumbele ambavyo ni utekelezaji wa miradi ya kimkakati ya kufua umeme na kuyafikishia umeme wa gridi ya Taifa maeneo ambayo haijafika.