November 25, 2022

CHANGAMOTO ZA UPUNGUFU WA UMEME KUPATIWA UFUMBUZI

 


Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) limeelezea sababu za uwepo wa upungufu wa umeme kuwa unasababishwa na ukame pamoja na matengenezo kinga na marekebisho makubwa kwenye vituo na mitambo, na kusababisha upungufu wa jumla ya megawati 300 hadi 350 za umeme kwa siku za hivi karibuni.

Akizungumza na waandishi wa vyombo vya habari hivi karibuni,  Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO, Bw.  Maharage Chande alisema upungufu wa umeme unasababishwa na ukame pamoja na matengenezo ya mitambo.

“Upungufu huu unasababishwa na mambo makubwa mawili, ukame mkubwa ambao nchi yetu inapitia na matengenezo kinga na marekebisho makubwa ya mitambo ambayo ni lazima yafanyike” alifafanua Bw. Chande.

Aidha, Bw. Chande aliviainisha vituo vya kufua umeme vilivyoathiriwa na ukame ambavyo ni  Kihansi kinachozalisha megawati 17 badala ya megawati 180 kwa hiyo megawati 163 hazizalishwi; Pangani kinachozalisha megawati 10 badala ya megawati 68 kwa hiyo megawati 58 hazizalishwi.

Vituo vingine ni Mtera kinachozalisha megawati 75 badala ya megawati 80 kwa hiyo megawati 5 hazizalishwi na Nyumba ya Mungu kinachozalishaji megawati 3 badala ya megawati 8 za umeme, kwa hiyo megawati 5 hazizalishwi. 

Vilevile, Bw. Chande alivitaja vituo vilivyo katika matengenezo kinga kuwa ni Kidatu kinachozalisha megawati 150 badala ya megawati 200, kwa hiyo megawati 50 hazizalishwi; Ubungo III kinachozalisha megawati 37 badala ya megawati 112, kwa hiyo megawati 75 hazizalishwi.

Kituo kingine ni Kinyerezi II kinachozalisha megawati 205 badala ya megawati 237, kwa hiyo megawati 32 hazizalishwi. Alifafanua jumla ya umeme ambao hauzalishwi kwa sababu ya ukame na matengenezo ni megawati 388 za umeme hadi kufikia 23 Novemba 2022.

Akieleza mipango ya muda mfupi ya kunusuru hali ya upungufu wa umeme, Bw. Chande  alisema ni kuharakisha matengenezo ya mtambo katika kituo cha Ubungo III ili kuingiza megawati 35 za umeme hadi kufikia leo, kuharakisha matengenezo ya mitambo miwili ya Ubungo III ili kuingiza megawati 40 za umeme mwishoni mwa mwezi Disemba 2022.

Sambamba na kukamilisha matengenezo ya mtambo mmoja wa kituo cha Kidatu ili kuingiza megawati 50 za umeme tarehe 30 Novemba 2022 pamoja na kuharakisha ufungaji wa mitambo miwili katika kituo cha upanuzi cha Kinyerezi I ili kuingiza megawati 90 za umeme kabla ya mwisho wa mwezi Disemba 2022.

“Iwapo matengenezo haya yatakamilika  kama yalivyopangwa, yatatupatia jumla ya megawati 277 kwenye uzalishaji na kupunguza kadhia hii ya umeme,” alisisitiza Bw. Chande.

Aidha, Bw. Chande alisema juhudi za muda wa kati  ni ukamilishaji wa ufungaji wa mtambo mwingine katika kituo cha upanuzi cha Kinyerezi I ili uanze kufanya kazi ili tuingize megawati 90 za umeme kwenye uzalishaji ifikapo mwezi Februari 2023 na kufikisha jumla ya megawati 337 za umeme.

Akihitimisha, Mkurugenzi Mtendaji alisema jitihada za muda mrefu ni kuharakisha ujenzi wa bwawa la Julius Nyerere.

“Hatua za muda mrefu ambazo ni zaidi ya miezi 12 mpaka 18, ni matumaini yetu, nguvu zetu na nia yetu bwawa la Julius Nyerere likamilike ili upungufu wa umeme uwe umekwisha” alihitimisha Bw. Chande.


May 19, 2022

WAZIRI MAKAMBA AELEZA SABABU ZA KUKATIKA KWA UMEME NCHINI

 


Waziri wa Nishati Mhe. January Makamba leo Mei 19, 2022 ameshiriki ziara ya Mhe. Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Samia Suluhu Hassan Mkoani Tabora ambapo amewahakikishia wananchi kuimarika kwa hali ya upatikanaji wa umeme nchini kupitia uwekezaji wa miradi ya umeme inayoendelea.


Akitoa salamu za Wizara ya Nishati Waziri Makamba amesema upatikanaji wa nishati ya umeme unategemea mambo matatu muhimu ambayo ni uzalishaji, usafirishaji na usambazaji.

"Uhakika wa upatikanaji wa umeme unategemea uimara wa miundombinu ya usafirishaji na uzalishaji wa umeme unaotosheleza" amesema Mhe. Makamba.

Ameongeza kuwa changamoto kubwa ya upatikanaji wa umeme nchini inatokana na uwepo wa miundombinu chakavu na isiyotosheleza mahitaji.

Amesema kwa muda mrefu Serikali haikufanya uwekezaji kwenye maeneo ya uzalishaji na miundombinu unaoendana na wakati pamoja na mahitaji ya kutosheleza.

"Mfumo wetu wa gridi umeelemewa kutokana na uchakavu ambao unasababisha maeneo mengi ya nchi yetu umeme kufika ukiwa umefifia na mwingi unakuwa unapotea njiani" amesisitiza Mhe. Makamba.

Akielezea changamoto za umeme ambazo zinazikabili Wilaya za Urambo na Kaliua Mkoani Tabora, Waziri Makamba amesema tatizo la kukatika kwa umeme katika Wilaya hizo zinatokana na njia ya umeme kutembea umbali mrefu takribani umbali wa kilometa 1,200.

"Tangu nchi yetu ipate uhuru mahitaji ya umeme yamekuwa yakiongezeka kila wakati, katika kipindi cha miezi sita iliyopita tumevunja rekodi ya mahitaji ya umeme mara nne, tumefikia mahitaji ya megawati 1,336 kiwango ambacho hakijawahi kufikiwa.

Amesisitiza hii inamaanisha shughuli za uchumi zinaongezeka kwa watu kufungua biashara na uwekezaji katika viwanda.

Kuhusu kutatua changamoto ya kukatika kwa umeme Waziri Makamba amesema Serikali imeweka mpango wa kurekebisha gridi wenye thamani ya takribani dola bilioni 1.9.

Mpaka sasa Serikali tayari imeshatenga kiasi cha shilingi bilioni mia 500  kwa mwaka ujao wa fedha 2022/2023 kutekeleza miradi mbalimbali itakayosaidia kuimarisha hali ya upatikanaji umeme kwenye gridi ya Taifa.

May 7, 2022

TANESCO KUOKOA TAKRIBANI BIL.1.7 NGORONGORO

 

Serikali ya Tanzania kupitia Shirika la Umeme nchini (TANESCO) imekamilisha ujenzi wa mradi wa umeme wenye thamani ya shilingi bil. 2.9 wa kuunganisha Wilaya ya Ngorongoro kwenye grid ya taifa.


Awali Wilaya ya Ngorongoro ilitumia umeme wa jenereta ambao ulikuwa ukigharimu kiasi cha bil.1.7 kama gharama za uendeshaji kwa mwaka,huku makusanyo ya wilaya ya ngorongo yakiwa ni Mil.374 kwa mwaka.

Akizindua umeme  huo wa gridi katika Wilaya ya Ngorongoro  Halmashauri ya mji mdogo wa Loriondo Mei 06, 2022, Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Mhe:John Mongela amesema TANESCO imekuwa ikifanya kazi kubwa katika kuwafikishia huduma ya umeme wananchi na uboreshaji wa miundombinu.

"Leo tunapozindua umeme gridi ya Taifa ni ushahidi tosha wa kazi kubwa wanayoifanya TANESCO, tumeona mradi huu ukikamilika ndani ya muda mfupi" amesema Mhe. Mongela.

Awali akitoa taarifa ya utekelezaji wa mradi, Meneja wa TANESCO Mkoa wa Arusha, Mhandisi Herini  Mhina amesema mradi huo ulianza kutekelezwa Septemba 25, 2021 na umekamilika Mai 04, 2022, ikiwa ni takribani miezi 7 mpaka kukamilika kwake.

Ameongeza kuwa kuunganisha Wilaya ya Ngorongoro na gridi ya Taifa kutachochea ukuaji wa uchumi kwa wananchi hao.

"Sasa Wilaya ya Ngorongoro inaenda kuwa na umeme wa uhakika na unaotabirika, jambo kubwa zaidi ni  kulipunguzia Shirika na Taifa  gharama kubwa za kuzalisha umeme wa kutumia mafuta ya dizeli" amesema Mha. Mhina.

Mradi huo umetekelezwa na TANESCO kwa kutumia wataalamu wake wa ndani, unahusisha usimikwaji wa nguzo za zege 686 pamoja na za miti 220 zenye urefu wa mita 13 na ni sehemu ya mkakati endelevu wa Shirika kwenye kuimarisha huduma ya umeme katika maeneo mbalimbali nchini.

February 11, 2022

MABORESHO KWENYE VISIMA VYA GESI SONGOSONGO YAKAMILIKA

 


Shirika la umeme Tanzania (TANESCO)limetangaza kukamilika kwa siku kumi za matengenezo ya mifumo katika visima vya gesi vilivyopo Songosongo jana Februari 10, 2022.

Maboresho hayo muhimu ambayo yalilenga kuongeza ujazo wa gesi ambao utakidhi mahitaji ya mitambo inayoongezwa kwenye vituo vya kuzalisha umeme vya Kinyerezi I itakayozalisha megawati 185 na Ubungo III megawati 112 na hivyo kupelekea kuongeza uzalishaji katika mfumo wa gridi kwa megawati 297.

Akitoa taarifa kwa umma leo Februari 11, 2022 Msemaji wa TANESCO, Martin Mwambene amesema kuwa Shirika hilo lilifanikiwa kutumia fursa ya matengenezo hayo kwenda sambamba na maboresho ya miundombinu ya umeme kwenye baadhi ya maeneo nchini ambayo yatasaidia huduma ya umeme kuendelea kuimarika. 

"Kutokana na mapungufu katika uzalishaji uliotokea mwaka jana kwasababu ya ukame, tuliandaa mkakati wa muda mfupi na muda mrefu na moja ya mikakati hiyo ni kuongeza uwezo wa kituo cha Kinyerezi I kutoka megawati 150 hadi 350 na kuongeza kituo cha Ubungo III kwa megawati 112" amesema Mwambene.  

Aliongeza kuwa Shirika linawashukuru wateja wake kwa uvumilivu katika kipindi chote cha siku kumi za matengenezo kilichopelekea mapungufu ya huduma ya umeme kwenye baadhi ya maeneo nchini.
  
Zoezi la matengenezo katika visima vya gesi vya Songosongo lilianza Februari 01 hadi 10, 2022 na kukamilika ndani ya wakati kama ilivyopangwa.

January 31, 2022

MAHARAGE AWATOA HOFU WATANZANIA KUHUSU UPATIKANAJI WA UMEME KATIKA KIPINDI CHA MATENGENEZO YA VISIMA VYA GESI ASILIA


Shirika la umeme Tanzania TANESCO limewatoa hofu wateja wake kuhusu hali ya upatikanaji umeme nchini wakati wa uboreshaji wa mfumo wa gesi asilia kwenye visima vya gesi vya TPDC(Tanzania Petroleum Development Company) na PAET(Pan African Energy Tanzania) kama yalivyotangazwa kuanza tarehe 1 hadi 10 mwezi huu.


Akifafanua kuhusu matengenezo hayo leo Januari 30,2022 wakati wa ziara aliyoifanya na waandishi wa habari kwenye kituo cha kupoza umeme cha kunduchi jijini Dar es salaam Maharage amesema nchi haitakua gizani na kwamba hakuna maeneo yatakayoathirika kwa siku zote kumi mfululizo kwa kukosa umeme.

‘‘Visima vile vya gesi asilia si vya TANESCO ni vya TPDC, SONGAS na PAET sisi ni wateja tunaochukua gesi kutoka kwao na ili wao watupatie nishati hiyo zaidi ni lazima kufanya maboresho ndani ya siku hizo 10 tulizozitangaza, hakuna eneo litaathirika zaidi ya siku 3 kwa kukosa umeme ndani ya siku hizo kumi za kupisha matengenezo na tayari tumeshatoa ratiba kwa maeneo yote yatakayoathirika kwa kila mikoa husika nchi nzima.’’amefafanua Maharage.

Aidha amesema sambamba na matengenezo ya visima hivyo Shirika litaendelea na maboresho yake na matengenezo mbalimbali  kwenye miundombinu yake ndani ya  muda wa siku 10 katika maeneo yote nchini ili kuhakikisha matengenezo yatakapokamilika huduma ya umeme inarejea katika hali yake ya kawaida.

Katika hatua nyingine Mkurugenzi huyo amesema kazi ya kuongeza uwezo wa kupokea na kupoza umeme katika kituo  cha kunduchi kilichoko eneo la Salasala jijini Dar es salaam iko ukingoni na tayari transforma mpya yenye ukubwa wa MVA 195 imekamilika kufungwa.

‘‘Transforma hii inategemewa kuwashwa ili kuanza kutumika wakati wa kipindi cha matengenezo ya visima vya gesi na umeme kama nilivyozungumza wiki ya jana’’ amesema Maharage.

Akieleza kwa undani faida za transforma hiyo kwa wateja wanaohudumiwa na kituo hicho Meneja mkoa wa Kinondoni kaskazini Mhandisi Regina Mvungi amesema  transforma hiyo itasaidia kuondoa matatizo ya umeme kucheza, kuwa mdogo na kuboresha hali ya upatikanaji umeme kuwa ya kutabirika na ya uhakika.

Vilevile faida zingine ni itasaidia wateja kutokosa huduma pindi transforma moja itakapopata hitilafu tofauti na hali ilivyokua hapo awali na kuwezesha mikoa mingine ya Kitanesco kama Kinondoni kusini kuwapa wateja huduma wanapokuwa na matengenezo  mbalimbali ya umeme.

Kituo cha kupokea na kusambaza umeme cha kunduchi kilianzishwa mwaka 1995 ambapo kutokana na ongezeko la mji kukua kwa kasi na uhitaji wa umeme lilazimu TANESCO kununua transforma mpya kubwa itakayosaidia kuimarisha hali ya upatikanaji umeme kwenye maeneo mbalimbali ya jiji la Dar es salaam.

January 28, 2022

TANESCO KUFANYA MABORESHO KWENYE VITUO VYAKE VYA UZALISHAJI UMEME VYA KINYEREZI I NA UBUNGO III


Katika jitihada za kuboresha upatikanaji wa umeme nchini, Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO), linaendelea na maboresho kwenye vituo vyake vya uzalishaji umeme vya Kinyerezi I itakayozalisha megawati 185 na Ubungo III megawati 112.


Akizungumza na wanahabari leo Januari 28, 2022 Mkurugenzi mkuu wa Shirika hilo, Maharage Chande amesema mpaka sasa uzalishaji kutoka mitambo ya Ubungo III umefikia Megawati 60 ambazo tayari zimeunganishwa kwenye gridi ya Taifa.

Amesema kwa sasa kazi ya kupanua kituo cha Kinyerezi I inaendelea na megawati 70 za awali zitaingia kwenye mfumo wa gridi mwezi Aprili 2022 na ifikapo mwezi Agosti 2022 kazi hiyo itakuwa imekamilika na kupelekea Kituo cha Kinyerezi I ambacho sasa kinazalisha megawati 150 kuwa na uwezo wa kuzalisha megawati 335.

‘‘Mitambo hii inayoongezwa ili iweze kuzalisha umeme, inapelekea mahitaji ya gesi asilia kuongezeka ambapo inalazimu kufanya uboreshaji wa mfumo wa gesi kwenye mifumo ya TPDC (Tanzania Petroleum Development Company) na PAET (Pan African Energy Tanzania)’’ amesema Maharage.

Aliongeza kuwa zoezi la uboreshaji litafanyika kwenye visima vya gesi vilivyopo Songosongo kuanzia tarehe 01 hadi 10 Februari 2022, ambapo kukamilika kwake kutahakikisha gesi  ya ziada inayohitajika inapatikana.

Hivyo utekelezaji wa maboresho hayo utapelekea mapungufu ya gesi kwenye mitambo ya kuzalishia umeme wa gesi asilia na kulazimika kuzimwa kwa baadhi ya mitambo ili kupisha zoezi hilo muhimu.

Sambamba na matengenezo hayo, hali hiyo itasababisha upungufu wa uzalishaji umeme na kuathiri baadhi ya maeneo, amesema wananchi watapata taarifa za makatizo ya umeme kama zitakavyotolewa na mikoa husika.

Maboresho hayo kwenye vituo vya vya uzalishaji umeme vya Kinyerezi I na Ubungo III yatasaidia kuimarisha hali ya upatikanaji umeme nchini na kupunguza malalamiko ya wateja ya kutokuwa na umeme wa uhakika na unaotabirika.



January 15, 2022

TANESCO KUENDELEA KUUNGANISHA UMEME KWA GHARAMA YA ELFU 27,000 MAENEO YA VIJIJINI

 

                             Meneja Mwandamizi Kanda ya Kati, Mhandisi Frank Chambua

Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) limewahakikishia wananchi wa maeneo ya vijijini kuendelea kupata huduma ya umeme kwa gharama ya shilingi elfu 27.


Hayo yamesemwa na Meneja Mwandamizi Kanda ya Kati, Mhandisi Frank Chambua leo Januari 15, 2022 katika Kijiji cha Kigwe Mkoani Dodoma, alipokuwa katika ziara ya kuelimisha na kuhamasisha wananchi wa eneo hilo kuunganisha huduma ya umeme.

"Tumekuja hapa kuwahakikishia wananchi wa vijijini tunaendelea kuwaunganisha kwa bei ya shilingi elfu 27 kupitia miradi inayotekelezwa na TANESCO" amesema Mhandisi Chambua.

Alifafanua kuwa,Serikali  imefadhili miradi ya umeme kwenye maeneo ya vijijini hivyo wananchi wanatakiwa kulipia elfu 27 ambayo inajumuisha kodi ya ongezeko la thamani yaani (VAT).

Mkutano huo pia ulienda sambamba na elimu kwa wateja iliyohusu kuelimisha uma taratibu sahihi zinazotakiwa kufuatwa kwenye kupata huduma ya umeme.

Ametoa wito kwa wananchi wa Mkoa wa Dodoma kusaidia kulinda miundombinu ya umeme hasa kipindi wanapoandaa mashamba na kuacha kuchoma nguzo moto.

Kwa upande wake Kaimu Meneja wa TANESCO Wilaya ya Bahi, Hassan A. Hassan amesema wanaendelea kuwaunganisha wateja wote wa maeneo ya vijijini kwa shilingi elfu 27.

"Tunaendelea kuwaunganishia wateja kwa elfu 27, leo tuna idadi ya wateja 16 ambao tutawaunganishia umeme, lakini pia tunahamasisha wananchi kuzidi kuomba kupata huduma ya umeme" amesema Hassan.

Kwa Mkoa wa Dodoma Serikali imewekeza jumla ya shilingi bilioni 195.5 kwa ajili ya kutekeleza miradi ya kuunganisha umeme. Mkoa huo una jumla ya vijiji 581 ambapo mpaka sasa takribani vijiji 422 vimefikiwa na huduma ya  umeme na vilivyobaki ni 159 ambavyo wakandarasi wanaendelea na kazi ya kuunganisha huduma hiyo.






September 26, 2021

TANESCO MPYA IMEZALIWA LEO, TUNATAKA IENDESHWE KIBIASHARA- Waziri Makamba

 

Waziri wa Nishati, Mhe. January Makamba amesema ni wakati sasa Shirika la Umeme Tanzania TANESCO kuanza kujiendesha kibiashara, kwa ufanisi ili kuchangia uchumi wa Taifa.

Mhe. Makamba amesema hayo leo Septemba 26, 2021 wakati akizungumza na Mameneja wa TANESCO wa ngazi ya Kanda, Mikoa, Wilaya na Makao Makuu. 

Aidha Mhe. Makamba amewatambulisha Wajumbe wa Bodi ya TANESCO wakiogozwa na Mwenyeki, Bw. Omari Issa, pamoja na Mkurugenzi Mtendaji, Bw. Maharage Chande, walioteuliwa Septemba 25, 2021 na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan.

Wajumbe wa Bodi ya TANESCO waliotambulishwa ni pamoja na Bw. Nehemia Mchechu, Bi. Zawadia Nanyaro, Bw. Lawrence Mafuru, Mhandisi Cosmas Masawe, Balozi Mwanaidi Maajar, Mhandisi Abdallah Hashim,  Bw. Abubakar Bakhresa na Bw. Christopher Gachuma.

Mhe. Makamba amesema Bodi iliyochaguliwa ina wajumbe kutoka nyanja mbalimbali na watasaidia Shirika kufikia malengo.

 "Tunataka baada ya miaka mitatu Shirika liingie katika orodha ya mashirika bora, yenye thamani na yanayoheshimika Afrika" alisema Mhe. January Makamba

Naye Mwenyekiti wa Bodi ya TANESCO, Bw. Omari Issa, amesema atahakikisha Bodi inafanya kazi na kutimiza malengo yake kwa kufuatilia kwa karibu utekelezaji wa malengo na uwajibikaji.

 Mkurugenzi Mtendaji, Bw. Maharage Chande, ameeleza vipaumbele ambavyo ni masilahi ya rasilimaliwatu, Wateja wa Shirika na utekelezaji wa mipango, hivyo ameomba ushirikiano kutoka kwa wafanyakazi wa TANESCO.

"Nimhakikishie Mhe. Waziri tutahakikisha tunarudisha heshima ya Shirika na ufanisi kupitia ushirikiano wenu, hakuna Shirika lolote linalotoa huduma ya umeme zaidi yetu sisi, yamkini tuwape wateja wetu huduma wanayostahili", " alisema Bw. Maharage Chande

Meneja Mwandamizi Rasilimaliwatu, Bw. Francis Sangunaa, aliwahakikishia viongozi ushirikiano kwa niaba ya wafanyakazi wa TANESCO.
 



 

September 4, 2021

MIRADI YA KIMKAKATI YA NISHATI ITAKAMILIKA KWA WAKATI

 

Naibu Katibu Mkuu Nishati, Bw. Kheri Mahimbali amesema miradi yote ya kimkakati ya umeme inayotekelezwa na Serikali kupitia TANESCO itakamilika kwa wakati.

Bw. Mahimbali ameyasema hayo leo Septemba 03, 2021 katika ziara ya Sekretarieti ya Baraza la Mawaziri, kukagua vituo vya kuzalisha umeme kwa gesi vya Kinyerezi.

Amesema ziara ilijikita zaidi kwenye mradi wa Julius Nyerere, ambapo Sekretarieti iliweza kufahamu hatua zote za kuzalisha umeme hadi kuusafilisha.

"Leo tumewaonesha Kinyerezi complex ambayo ina Kinyerezi I, Kinyerezi I Extension pamoja na Kinyerezi ll" amesema Bw. Mahimbila.

Ametoa pongezi kwa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inayoongozwa na Rais, Mhe. Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa inayoifanya katika kuendeleza miradi ya umeme nchini.

Sekretarieti ya Baraza la Mawaziri inahitimisha leo ziara ya siku tatu kukagua miradi ya umeme, ziara ilianzia kwenye kituo cha kupokea na kupoza umeme cha Zuzu Jijini Dodoma, njia ya umeme itakayojengwa hadi Chalinze na mradi wa kufua umeme kwa maji wa Julius Nyerere.





 

September 3, 2021

Mkandarasi JNHPP ameshalipwa trilioni 2.7

 


 Mkurugenzi Mtendaji TANESCO, Dkt. Tito Mwinuka amesema Mkandarasi anaetekeleza mradi wa Julius Nyerere (JNHPP) Mw 2115 ameshalipwa jumla ya shilingi trilioni 2.7 kulingana na mpango kazi kati ya shilingi trilioni 6.5 anazotakiwa kulipwa hadi kukamilika kwa mradi.

Dkt. Mwinuka ameyasema hayo leo Ijumaa Septemba 03, 2021 katika ziara ya Sekretarieti ya Baraza la Mawaziri, Wafanyakazi wa Ofisi ya Rais Ikulu na Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora.

Kwa upande wake Karani wa Baraza la Mawaziri, Bw. Nsubili Joshua amesema ameongozana na Maafisa wa Sekritarieti ili kujionea kazi inavyoendelea JNHPP.

Amesema mradi wamekuwa wakiufahamu kwenye makaratasi hivyo wamefika kujionea hali halisi na kuona kinachoendelea.

Ameongeza kuwa wameona mambo makubwa ambayo hawayajatarajia na kutoa pongezi kwa viongozi wakuu Serikalini kwa kuutekeleza mradi huo.

Awali akieleza lengo la ziara hiyo, Katibu Mkuu Ofisi ya Rais Menejimenti ya utumishi wa umma, Bw. Lauren Ndumbaru amesema wamefanya ziara katika mradi na watumishi wa umma wa ngazi zote ili watumishi waweze kuona na kuthamini kazi ambayo Serikali inafanya katika ujenzi wa miradi ya kimkakati.

"Naamini kabisa mradi wa Julius Nyerere ukikamilika utaleta maendeleo makubwa katika Nchi yetu, niombe watumishi wa umma wafanye kazi kwa bili na waendelee kuiunga mkono Serikali ili tuone matokeo mapema" amesema Bw. Ndumbalo

Naibu Katibu Mkuu Nishati, Bw. Kheri Mahimbali amesema Wizara ya Nishati imefarijika kutokana na Ofisi zote mbili kuridhishwa na utekelezaji wa mradi wa Julius Nyerere.

"Tunamshukuru Rais Samia Hassan kwa kuendelea kuuangalia mradi huu kwa jicho la kipekee kabisa, tunapata pesa za kuendeleza mradi kwa wakati na usimamizi mzuri, tutaendelea kuusimamia na kuhakikisha mradi huu unakamilika kwa wakati" amesema Bw. Mahimbila.