May 19, 2022

WAZIRI MAKAMBA AELEZA SABABU ZA KUKATIKA KWA UMEME NCHINI

 


Waziri wa Nishati Mhe. January Makamba leo Mei 19, 2022 ameshiriki ziara ya Mhe. Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Samia Suluhu Hassan Mkoani Tabora ambapo amewahakikishia wananchi kuimarika kwa hali ya upatikanaji wa umeme nchini kupitia uwekezaji wa miradi ya umeme inayoendelea.


Akitoa salamu za Wizara ya Nishati Waziri Makamba amesema upatikanaji wa nishati ya umeme unategemea mambo matatu muhimu ambayo ni uzalishaji, usafirishaji na usambazaji.

"Uhakika wa upatikanaji wa umeme unategemea uimara wa miundombinu ya usafirishaji na uzalishaji wa umeme unaotosheleza" amesema Mhe. Makamba.

Ameongeza kuwa changamoto kubwa ya upatikanaji wa umeme nchini inatokana na uwepo wa miundombinu chakavu na isiyotosheleza mahitaji.

Amesema kwa muda mrefu Serikali haikufanya uwekezaji kwenye maeneo ya uzalishaji na miundombinu unaoendana na wakati pamoja na mahitaji ya kutosheleza.

"Mfumo wetu wa gridi umeelemewa kutokana na uchakavu ambao unasababisha maeneo mengi ya nchi yetu umeme kufika ukiwa umefifia na mwingi unakuwa unapotea njiani" amesisitiza Mhe. Makamba.

Akielezea changamoto za umeme ambazo zinazikabili Wilaya za Urambo na Kaliua Mkoani Tabora, Waziri Makamba amesema tatizo la kukatika kwa umeme katika Wilaya hizo zinatokana na njia ya umeme kutembea umbali mrefu takribani umbali wa kilometa 1,200.

"Tangu nchi yetu ipate uhuru mahitaji ya umeme yamekuwa yakiongezeka kila wakati, katika kipindi cha miezi sita iliyopita tumevunja rekodi ya mahitaji ya umeme mara nne, tumefikia mahitaji ya megawati 1,336 kiwango ambacho hakijawahi kufikiwa.

Amesisitiza hii inamaanisha shughuli za uchumi zinaongezeka kwa watu kufungua biashara na uwekezaji katika viwanda.

Kuhusu kutatua changamoto ya kukatika kwa umeme Waziri Makamba amesema Serikali imeweka mpango wa kurekebisha gridi wenye thamani ya takribani dola bilioni 1.9.

Mpaka sasa Serikali tayari imeshatenga kiasi cha shilingi bilioni mia 500  kwa mwaka ujao wa fedha 2022/2023 kutekeleza miradi mbalimbali itakayosaidia kuimarisha hali ya upatikanaji umeme kwenye gridi ya Taifa.

May 7, 2022

TANESCO KUOKOA TAKRIBANI BIL.1.7 NGORONGORO

 

Serikali ya Tanzania kupitia Shirika la Umeme nchini (TANESCO) imekamilisha ujenzi wa mradi wa umeme wenye thamani ya shilingi bil. 2.9 wa kuunganisha Wilaya ya Ngorongoro kwenye grid ya taifa.


Awali Wilaya ya Ngorongoro ilitumia umeme wa jenereta ambao ulikuwa ukigharimu kiasi cha bil.1.7 kama gharama za uendeshaji kwa mwaka,huku makusanyo ya wilaya ya ngorongo yakiwa ni Mil.374 kwa mwaka.

Akizindua umeme  huo wa gridi katika Wilaya ya Ngorongoro  Halmashauri ya mji mdogo wa Loriondo Mei 06, 2022, Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Mhe:John Mongela amesema TANESCO imekuwa ikifanya kazi kubwa katika kuwafikishia huduma ya umeme wananchi na uboreshaji wa miundombinu.

"Leo tunapozindua umeme gridi ya Taifa ni ushahidi tosha wa kazi kubwa wanayoifanya TANESCO, tumeona mradi huu ukikamilika ndani ya muda mfupi" amesema Mhe. Mongela.

Awali akitoa taarifa ya utekelezaji wa mradi, Meneja wa TANESCO Mkoa wa Arusha, Mhandisi Herini  Mhina amesema mradi huo ulianza kutekelezwa Septemba 25, 2021 na umekamilika Mai 04, 2022, ikiwa ni takribani miezi 7 mpaka kukamilika kwake.

Ameongeza kuwa kuunganisha Wilaya ya Ngorongoro na gridi ya Taifa kutachochea ukuaji wa uchumi kwa wananchi hao.

"Sasa Wilaya ya Ngorongoro inaenda kuwa na umeme wa uhakika na unaotabirika, jambo kubwa zaidi ni  kulipunguzia Shirika na Taifa  gharama kubwa za kuzalisha umeme wa kutumia mafuta ya dizeli" amesema Mha. Mhina.

Mradi huo umetekelezwa na TANESCO kwa kutumia wataalamu wake wa ndani, unahusisha usimikwaji wa nguzo za zege 686 pamoja na za miti 220 zenye urefu wa mita 13 na ni sehemu ya mkakati endelevu wa Shirika kwenye kuimarisha huduma ya umeme katika maeneo mbalimbali nchini.