February 27, 2019

Katibu Mkuu Nishati ahitimisha ziara ya kikazi kukagua miradi ya umeme

Katibu Mkuu Wizara ya Nishati Dkt. Hamisi Mwinyimvua, amehitimisha ziara ya kikazi ya siku tatu jijini Dar es Salaam ya kukagua miradi mbalimbali ya umeme inayotekelezwa na TANESCO kwa kuwahakikishia wakazi wa Kigamboni ifikapo katikati ya mwezi Machi, 2019, kero ya umeme itakuwa imemalizika kabisa.

Dkt. Mwinyimvua ametoa hakikisho hilo baada ya kutembelea kituo cha kupoza na kusambaza umeme cha Kurasini ambacho amesema ujenzi wake umekamilika na Machi 6, kitawashwa kwa mara ya kwanza.

"Nimetembelea Kurasini ambapo ile sub station mpya kwakeli imekamilika na kilichobaki ni kuvusha nyaya kutoka Kurasini kuleta Kigamboni kazi ambayo itakuwa imekamilika ifikapo tarehe 6 Machi." Alisema na kuongeza kuwa tarehe 8 au 10 wataalamu watafanya uwashaji mitambo.

Aidha, ziara ya Dkt. Mwinyimvua alifanya ziara hadi eneo la Dege ambako TANESCO inajenga kituo cha kupoza na kusambaza umeme kwenye eneo lote la Kigamboni ambalo kwa mujibu wa Katibu Mkuu, eneo hilo linakuwa kwa kasi na hivyo Serikali kupitia TANESCO lazima ichukue tahadhari kwa kuweka miundombinu tayari ili pakitokea uhitaji huduma iweze kuwafikia wananchi bila shida yoyote.

Kwa mujibu wa Meneja wa ujenzi wa kituo cha Dege, Mhandisi Neema Mushi, kazi ya ujenzi wa kituo hicho kwa sehemun kubwa imekamilika miundombinu yake na kwamba kinachosubiriwa na kuletwa kwa mitambo ili iweze kufungwa.
 Katibu Mkuu Wizara ya Nishati, Dkt.Hamisi Mwinyimvua (kulia), na Kamishna wa Umeme na Nishati Jadidifu, Mhandisi Innocent Luoga, (kushoto), wakimsikilzia Meneja mradi wa ujenzi wa kituo cha kupoza na kusambaza umeme cha Dege, Kigamboni jijini Dar es Salaam, Mhandisi Neema Mushi
Moja ya minara mirefu ya kupitisha nyaya za umeme mkubwa wenye msongo wa 132 kV kuelekea ng'ambo ya pili ya Kigamboni kutoka Kurasini jijini Dar es Salaam, zikiwa tayari na baadhi yake zikionekana kufungwa nyaya.
Mkuu wa Miradi (anayeshughulikia usafirishaji) wa TANESCO, Mhandisi Frank Mashalo(kushoto), akifafanua jambo mbele ya Dkt. Mwinyimvua, (wapili kushoto), Kamishna wa Umeme na Nishati Jadidifu, Mhandisi Innocent Luoga, (wakwanza kulia) na Meneja Miradi wa TANESCO, Mhandisi Stephene Manda walipotembelea kituo cha kupoza na kusambaza umeme cha Kurasini jijini Dar es Salaam Februari 27, 2019.
Mkuu wa Miradi (anayeshughulikia usafirishaji) wa TANESCO, Mhandisi Frank Mashalo, akifafanua Zaidi kuhusu utayari wa kituo hicho.
Meneja wa Mkoa wa TANESCO Temeke, Mhandisi Jafari Mpina akieleza jambo mbele ya Dkt. Mwinyimvua.
Meneja Miradi wa TANESCO, Mhandisi Stephene Manda(kushoto), akielezea jinsi nyaya zitakavyovushwa kuelekea Kigamboni kutoka Kurasini.
Taswira ya maendeleo ya ujenzi wa kituo cha kupoza na kusambaza umeme cha Dege huko Kigamboni jijini Dar es Salaam kama kinavyoonekana leo Februari 27, 2019 ambapo kwa mujibu wa Meneja Mradi wa ujenzi wa kituo hicho, Mhandisi Neema Mushi, miundombinu ya kituo hicho imekamilika na kinachosubiriwa na mashine ili ziweze kufungwa.
Taswira ya maendeleo ya ujenzi wa kituo cha kupoza na kusambaza umeme cha Dege huko Kigamboni jijini Dar es Salaam kama kinavyoonekana leo Februari 27, 2019 ambapo kwa mujibu wa Meneja Mradi wa ujenzi wa kituo hicho, Mhandisi Neema Mushi, miundombinu ya kituo hicho imekamilika na kinachosubiriwa na mashine ili ziweze kufungwa.
Mobile; +255 646-453/+255-653

February 26, 2019

KATIBU MKUU WIZARA YA NISHATI, DKT. MWINYIMVUA AWAPONGEZA WATAALAMU WA TANESCO

Katibu Mkuu Wizara ya Nishati, Dkt. Hamisi Mwinyimvua, amewapongeza wataalamu wa Shirika TANESCO kwa kazi kubwa ya kuhakikisha umeme unawafikia Wateja.

Dkt. Mwinyimvua ametoa pongezi hizo Februari 26, 2019 wakati alipotembelea vituo vya kufua umeme wa gesi  vya Ubungo I, Ubungo II, Songas lakini pia kuona kazi ya kufunga transfoma mpya kwenye Kituo Kikuu cha kupoza na kusambaza umeme cha Ubungo.  

Dkt. Mwinyimvua ambaye alifuatana na Kaimu Kamishna wa Umeme na Nishati Jadidifu, Mhandisi Innocent Luoga, alisema “Tunazitambua changamoto zinazowakabili, lakini niwapongeze kwa kazi nzuri mnayofanya ya kuhakikisha huduma ya umeme inawafikia wateja”.

Akitoa taarifa ya Kituo cha kufua umeme utokanao na gesi asilia cha Ubungo II, Meneja wa kituo Mhandisi Lucas Busunge, alisema kituo hicho kina mashine tatu za kufua umeme kila moja ikizalisha Megawati 43 na hivyo kufanya jumla ya Megwati 129.

Adha kwa sasa kituo hicho kiko kwenye matengenezo makubwa ya kinga yaani (Preventive maintanence), kwa jina la kitaalamu matengenezo hayo huitwa Level C Inspection na hufanyika baada ya mitambo kutembea zaidi ya masaa 40,000 tangu kituo kianze kuzalisha umeme, alisema Mhandisi Busunge.

“Matengenezo haya yatahusisha mitambo yote mitatu na mtambo wa kwanza ulianza kutengenezwa Januari 9, 2019 katika mtambo namba mbili na yatafanyika kwa awamu kwa kuzima mtambo mmoja baada ya mwingine hadi yatakapokamilika na tunatarajia kazi hii ya kufanya matengenezo itakamilika Juni 5, 2019.” Alifafanua.

Matengenezo  hayo yanaambatana na marekebisho ya kufanya mitambo isizime kwa masaa 40 kila baada ya umeme wa Gridi ya Taifa kukatika kama ilivyo hivi sasa ambapo Gridi ya Taifa ikitoka basi mitambo ina block kwa masaa 40 kabla ya kurejea katika hali yake ya kawaida.

“Marekebisho hayo yataiwezesha mitambo kuweza kuanzisha Gridi kama ilivyo katika vituo vya Kidatu kuweza kurejesha umeme kwa haraka. Hivyo marekebisho haya yatawezesha mitambo kurejesha umeme kwa haraka jijini Dar es Salaam wakati umeme wa Gridi ya Taifa unapokatika.” Alibainisha Mhandisi Busunge.

Katika siku za hivi karibuni kunekuwepo na changamoto ya upatikanaji umeme kwa wakati wote baadhi ya maeneo ya jiji la Dar es Salaam ambapo imeelezwa kuwa sehemu kubwa ya wakazi wa Dar es Salaam, Zanzibar na Pwani hutegemea Kituo Kikuu cha kupoza na kusambaza umeme cha Ubungo ambacho kina transfoma mbili kubwa kila moja ina uwezo wa kusukuma Megawati 110 kila moja na kufanya jumla ya Megawati 220, lakini pia kuna Megawati zingine 300 kutoka vyanzo vingine vya Songas, Ubungo II na Tegeta na kufanya jumla ya Megawati 520 wakati mahitaji halisi ya Dar es Salaam, Zanzibar na Pwani ni Megawati 570 na hapo kunakuwa na upungufu wa Megawati 50.
Kutokana na upungufu huo, Serikali kupitia Shirika la Umeme Nchini TANESCO imechukua hatua ya kununua Transfoma kubwa yenye uwezo wa kusukuma takribani Megawati 240 kutoka kwenye msongo wa kilovoti 220 kuelekea Msongo wa kilovoti 132 ili kuongezea nguvu umeme unaotumika katika mikoa ya Dar es Salaam, Zanzibar na Pwani, ameongeza Meneja Miradi wa TANESCO Mhandisi Stephene Manda.

“Tunao umeme wa kutosha kilichokuwa kinasumbua ni namna ya kuushusha umeme huo wa msongo wa kilovoti 220 na kuushusha hadi msongo wa kilovolti 132 na ndiyo kazi tunayofanya hivi sasa ya kufunga transfoma mpya ambayo itatatua changamoto hiyo.” Alisema Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati Mhandisi Hamisi Mwinyimvua.

Pia Dkt. Mwinyimvua aliwapongeza TANESCO kwa ubunifu walioufanya wa kufanya marekebisho kwenye mitambo yake mitatu ya Kituo cha kufua umeme wa gesi asilia cha Ubungo II ambapo baada ya marekebisho hayo, umeme ukitoka kwenye Gridi ya Taifa, basi mitambo hiyo inaweza kuingilia kati na hivyo kulifanya jiji la Dar es Salaam na kuwa salama kwa maana ya kutoathirika kwa kutoka kwa Gridi ya Taifa.

KATIBU Mkuu Wizara ya Nishati, Dkt. Hamisi Mwinyimvua,(watatu kulia), akizungumza na vyombo vya habari mbele ya mashine (turbine) ya kufua umeme inayofanyiwa matengenezo makubwa ya kujilinda kwenye kituo cha kufua umeme wa gesi asilia cha Ubungo II, jijini Dar es Salaam. 
 Dkt.Mwinyimvua (wapili kushoto), na Kaimu Kamishna wa Umeme na Nishati Jadidifu, Mhandisi Innocent Luoga, (kulia), wakiongozwa na Meneja Miradi wa TANESCO, Mhandisi Stephene Manda, (kushoto), walipotembelea kuona transfoma hiyo.
 Hii ndiyo transfoma kubwa mpya yenye uwezo wa kusukuma umeme wa Megawati 240, ambayo inafungwa kwenye Kituo kikuu cha kupoza na kusambaza umeme cha Ubungo na hivyo kufanya kituo hicho kuwa na transfoma tata.
 Wataalamu wakiwa kwenye chumba cha SCADA wakifuatilia mwenendo wa umeme kutoka vyanzo na vituo mbalimbali vya umeme nchini. Kituo hiki kiko Ungungo.


 Meneja wa Kituo cha kufua umeme utokanao na gesi asilia cha Ubungo II, Mhandisi Lucas Busunge, (kushoto), akifafanua jambo mbele ya Katibu Mkuu, Dkt. Mwinyimvua (wapili kulia) na Kaimu Kamishna wa Umeme na Nishati Jadidifu, Mhandisi Innocent Luoga, (watatu kushoto).

Mhandisi wa TANESCO ambaye anahudumu kwenye chumba cha udhibiti (control room) cha kituo kikuu cha kupoza na kusambaza umeme cha Ubungo akitoa maelezo kwa Katibu Mkuu na ujumbe wake, walipotembelea kituo hicho leo Februari 26, 2019.

KATIBU MKUU NISHATI ATEMBELEA MIRADI YA UMEME KINYEREZI

Katibu Mkuu Wizara ya Nishati, Dkt. Hamisi Hassan Mwinyimvua ametembelea Kituo cha kufua umeme wa Gesi Asilia Kinyerezi I extension na Kinyerezi II jijini Dar es Salaam.
Lengo la ziara yake alisema ni kuangalia maendeleo ya utekelezaji wa miradi ya Kinyerezi II na ule wa upanuzi wa Kinyerezi I (Kinyerezi I expansion)
Mradi wa Kinyerezi II ambao unazalisha kiasi cha Megawati 240 tayari umekamilika na umeme umekwishaingizwa kwenye Gridi ya Taifa.
“Tunashukuru kwamba tunaenda vizuri hasa Kinyerezi II ambayo kiukweli mradi umeshamalizika sasa hivi tunapata umeme kilichobaki ni masuala ya kuweka kila kitu sawa baina ya Mkandarasi na wataalamu wetu.” Alisema Dkt. Mwinyimvua baada ya kupokea taarifa ya miradi hiyo miwili toka kwa Meneja Miradi, Mhandisi Stephene Manda.
Alisema kwa upande wa mradi wa upanuzi Kinyerezi I, (Kinyerezi I extension) kazi imeanza ingawa kulikuwepo na ucheleweshwaji wa vifaa bandarini na kuagiza Uongozi wa TANESCO kukutana na taasisi zinazohusika na masuala ya kodi na utoaji mizigo bandarini ili kupanga utaratibu wa jinsi ya kulipa kodi mbalimbali bila ya kuathiri utoaji wa mizigo hiyo (vifaa na mitambo) bandarini.
“Nakumbuka mlipewa wito na Mheshimiwa Waziri wa Nishati, Dkt. Medard Kalemani akiwataka mjitahidi isifike mwezi wa nane, ikiwezekana hata mwezi wa tano muwe mmemaliza kazi.” Alisema.
Katika ziara hiyo, Katibu Mkuu alifuatana na Kamishna wa Nishati kutoka Wizara ya Nishati, Mhandisi Innocent Luoga wakati kwa upande wa Shirika la Umeme Tanzania TANESCO, waliongozwa na Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika hilo, Dkt. Tito Mwinuka.
Akitoa taarifa kwa Katibu Mkuu na ujumbe wake, Meneja Miradi wa TANESCO, Mhandisi Stephene Manda, alisema wakati Mradi wa Kinyerezi II Megawati 240 ambao umekamilika tangu Desemba mwaka jana (2018), mradi wa Kinyerezi I ambao unafanya kazi una Megawati 150 na ule wa kufanya upanuzi (Kinyeerzi I extension) utakuwa na Megawati 185 na kazi tayari imefikia asilimia 76%
“Tunategemea mtambo wa kwanza wa mradi huu wa upanuzi tutakuwa tumeuwasha ifikapo mwezi Mei, 2019 na kukamilika kabisa kwa mradi mzima itakuwa Agosti 2019.” Alibainisha Mhandisi Manda na kuongeza Jumla ya umeme utakaokuwa unazalishwa hapa Kinyerezi kufikia Agosti mwaka huu itakuwa Megawati 575.” Alisema
Akifafanua zaidi alisema kutoka pale Kinyerezi I Extension tutakuwa na extension ndogo ya kutoa umeme kwa ajili ya mradi wa SGR.
Katibu Mkuu Wizara ya Nishati, Dkt. Hamisi Hassan Mwinyimvua (katikati) na Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO Dkt. Tito Mwinuka (kulia), wakiongozwa na Meneja Miradi, Mhandisi Stephene Manda (kushoto), wakati Katibu Mkuu akikagua maendeleo ya mradi wa upanuzi wa kituo cha kufua umeme wa Gesi Kinyerezi I (Kinyerezi I expansion), jijini Dar es Salaam, Februari 25, 2019.
Katibu Mkuu Wizara ya Nishati, Dkt. Hamisi Hassan Mwinyimvua (watatu kulia), Kamishna wa Nishati, Mhandisi Innocent Luoga, (watano kulia), na Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO Dkt. Tito Mwinuka (wapili kulia), wakiongozwa na Meneja Miradi wa Shirika hilo. Mhandisi Stephene Manda (aliyenyoosha mikono) wakati Katibu Mkuu akikagua maendeleo ya mradi wa upanuzi wa kituo cha kufua umeme wa Gesi Kinyerezi I (Kinyerezi I expansion), jijini Dar es Salaam, Februari 25, 2019.
Katibu Mkuu pia alijionea kituo cha kupokelea gesi kikiwa tayari kwenye eneo la mradi huo.

KATIBU Mkuu Wizara ya Nishati, Dkt. Hamisi Hassan Mwinyimvua, akipatiwa maelezo.
Kamishna wa Nishati, Mhandisi Innocent Luoga(kushoto), akiwa na Mkandarasi eneo la mradi.
Katibu Mkuu Dkt. Mwinyimvua na ujumbe wake wakimsikiliza mkandarasi anayetekeleza mradi wa upanuzi Kinyerezi I, kuhusu mwenendo wa mradi huo.
Kiongozi wa zamu wa chumba cha udhibiti mitambo, kwenye mradi wa umeme wa gesi Kinyerezi II, Mhandisi Chidololo Enzi, (kulia) akitoa maelezo mbele ya Katibu Mkuu Wizara ya Nishati, Mhandisi Hamisi Hassan Mwinyimvua (katikati), alipotembelea kujihakikishia kukamilika kwa mradi huo unaozalisha Megawati 240.
Kiongozi wa zamu wa chumba cha udhibiti mitambo, kwenye mradi wa umeme wa gesi Kinyerezi II, Mhandisi Chidololo Enzi, (kulia) akitoa maelezo mbele ya Katibu Mkuu Wizara ya Nishati, Mhandisi Hamisi Hassan Mwinyimvua(kulia) na Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO Dkt. Tito Mwinuka (wapili kushoto).
Katibu Mkuu Wizara ya Nishati, Dkt. Hamisi Hassan Mwinyimvua (wapili kushoto), Kamishna wa Nishati, Mhandisi Innocent Luoga, (wakwanza kushoto), na Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO Dkt. Tito Mwinuka (wapili kulia), wakiongozwa na Meneja Miradi wa Shirika hilo. Mhandisi Stephene Manda (aliyenyoosha mkono) wakati Katibu Mkuu akikagua maendeleo ya mradi wa Kinyerezi II jijini Dar es Salaam Februari 25, 2019 ambapo alielezwa kuwa tayari umekamilika.
Hii ndiyo Kinyerezi II kama inavyoonekana Februari 25, 2019 wakati wa ziara ya Katibu Mkuu Nishati, Dkt. Mwinyimvua.




February 25, 2019

HALI YA UPATIKANAJI WA UMEME KATIKA JIJI LA DAR ES SALAAM

Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) linawaomba radhi Wateja wake wa Mkoa wa Dar es salaam kwa kukosa huduma ya umeme kwa siku za hivi karibuni kutokana na maboresho makubwa yanayohusisha matengenezo kinga ya mashine 3 za Kituo cha Ubungo II, pamoja na uwekaji wa transfoma kubwa la MVA 300 kwenye Kituo cha kupoza umeme cha Ubungo ili kukiongezea uwezo na kwenda sambamba na ukuaji wa mahitaji ya jiji la Dar es Salaam.

 Kabla ya matengenezo kuanza mnamo Januari 2019 Kituo hiki cha kupoza umeme cha Ubungo kimekuwa kinapokea umeme kutoka katika vituo vya Uzalishaji umeme vilivyopo upande wa msongo wa kilovolti 220 kupitia transfoma mbili zenye uwezo wa MVA 150 kila moja, zenye kupokea umeme wa msongo wa Kilovolti  220 na kuushusha hadi kuwa msongo wa Kilovolti 132  katika transforma namba sita na namba  saba za kituo cha Ubungo na  vituo vya uzalishaji umeme vilivyoungwa kwenye msongo wa kilovolti 132 ambavyo vimeungwa moja kwa moja kwenye mfumo mkuu wa usambazaji umeme  kwa Dar es Salaam na Zanzibar.

Kutokana na matengenezo yanayoendelea vituo vya uzalishaji umeme vilivyoungwa kwenye msongo wa kilovoti 132 na 33 vimekuwa nguzo kubwa ya upatikanaji wa umeme. Vituo hivyo ni Ubungo II na Tegeta.

Shirika kupitia wataalamu wake tayari limefanya jitihada kubwa za kupunguza athari za upungufu wa upatikanaji wa umeme kwa wakaazi wa Dar es salaam na Zanzibar kwa kufanya yafuatayo:

Mosi, Kufungua laini ya msongo wa kilovoti 132 kati ya Kilimanjaro na Hale: Hili hufanyika ili kutoruhusu umeme wa kutoka Dar es Salaam na Morogoro kwenda Kilimanjaro hivyo Mkoa huu kuchukulia kwenye upande wa msongo wa kilovolti 220 kutoka Arusha.

Pili , Kuwezesha upatikanaji wa umeme katika baadhi ya  maeneo ya Mkoa wa Dar es salaam, kwa kuunga baadhi ya njia za Usafirishaji  umeme kutoka Kituo cha Kinyerezi, Gongolamboto hadi Mbagala ili kuwezesha maeneo hayo kupata umeme bila kupitia kituo cha Ubungo  ambacho kipo katika matengenezo.

Tatu, Kufungua njia ya umeme ya kilovolti 132 itokayo Kituo cha Kunduchi   hadi Mlandizi na kuunga maeneo hayo katika njia ya umeme ya kilovolti 132 itokayo Morogoro ili kuwezesha jiji la Dar es salaam kuwa na umeme wa uhakika.

Nne, Kufungua laini ya msongo wa kilovolti 132 kati ya Ubungo na Chalinze upande wa Ubungo ili kutozihusisha transfoma za Ubungo kwenye mzigo wa mikoa mingine na hivyo kutumika kuhudumia  wateja wa  Dar es Salaam na Zanzibar pekee.
 Tunatarajia matengenezo haya yanayokwenda kwa awamu yatakamilika ifikapo mwezi Juni 2019.

TANESCO itaendelea kutoa taarifa ya Maendeleo ya kazi ya matengenezo ya kituo cha Ubungo yenye lengo la kuwezesha upatikanaji wa umeme wa uhakika Dar es salaam na Zanzibar kwa siku zijazo.


Imetolewa na:  Ofisi ya Uhusiano
                                TANESCO-Makao Makuu