September 28, 2018

Serikali inatarajia mzalishe umeme kupitia joto ardhi "Mheshimiwa Waziri Mkuu "

Waziri Mkuu wa Jamuhuri wa Muungano wa Tanzania Mhe. Majaliwa Kassim Majaliwa  akipata maelezo namna ambavyo TANESCO inawatumia watalamu wa Jiolojia katika kutekeleza miradi mbalimbali. 

NA SAMIA CHANDE, DODOMA

 Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Majaliwa Kassim Majaliwa amefungua kongamano la mwaka la Jumuiya ya Wanajiosayansi Tanzania (Tanzania Geological Society - TGS) Jijini Dodoma.

Alisema, watalamu wa Giolojia ni muhimu katika kueleta maendeleo ya Viwanda kupitia Nishati mbalimbali za umeme kama vile kuzalisha kwa kutumia Jotoardhi.

"Jotoardhi ni chanzo kizuri cha nishati kwa hivyo niwapongeze TANESCO kupitia kampuni tanzu ya TGDC, Serikali inatarajia hivi karibuni muanze kuzalisha umeme kupitia Jotoardhi", alisema Mhe. Majaliwa.

TANESCO imeshiriki katika kongamano hilo kupitia Kampuni tanzu ya Uendelezaji wa Jotoardhi Nchini (TGDC). Aidha, Mhe. Majaliwa alitembelea banda la TANESCO na kupatiwa taarifa mbalimbali kuhusu umuhimu wa Sekta ya Jiolojia katika uzalishaji, usafirishaji na usambazaji wa nishati ya umeme.

Akimuelezea Mheshimiwa Waziri Mkuu umuhimu wa jioloji katika utekelezaji wa miradi ya umeme, Mhandisi Eliaza Wangwe kutoka Idara ya Utafiti TANESCO, alisema tasnia ya jioloji ni muhimu katika utekelezaji wa miradi ya umeme katika hatua zote kuanzia utafiti, ujenzi na usimamizi. Aliongezea, TANESCO kupitia Kampuni Tanzu TGDC inaendelea kufanya tafiti mbalimbali ili kuwezasha uzalisha umeme utokanao na rasilimali ya jotoardhi.
"Jotoardhi ni nishati jadidifu, nafuu na endelevu inayoweza kutumika katika kuzalisha umeme na matumizi mengine kama vile kilimo, ukaushaji wa mazao na ufugaji wa samaki", alisema Mhandisi Wangwe.

 Kwa upande wake Meneja Mipango na Miradi kutoka TGDC Mhandisi Shakiru Kajugus, alisema Tanzania ina uwezo wa kuzalisha zaidi ya Megawati 5000 zitokanazo na jotoardhi.

 “Nchi yetu ina zaidi ya maeneo 50 yenye viashiria vya Jotoardhi ambapo maeneo hayo mengi yanapatikana katika Bonde la Ufa la Afrika Mashariki ambalo linapita hadi Kenya ambao tayari wanazalisha zaidi ya 700MW za Jotoardhi kwa sasa.” Mhandisi Kajugus.

 TGDC inaendelea na tafiti katika maeneo mbalimbali nchini kama vile eneo la Ziwa Ngozi lililoko Mkoani Mbeya ambapo ndipo yalipo makutano ya bonde la ufa la upande wa mashariki na lile la magharibi. Utafiti huo katika hatua ya uchorongaji visima vya majaribio ili kuthibitisha uwepo na kiwango cha rasilimali ya jotoardhi iliyopo katika eneo hilo.

Katika kukuza uchumi wa viwanda joto ardhi itatumika katika miradi mbalimbali kama kilimo na viwandani.




September 15, 2018

TANESCO KUOKOA ZAIDI YA SH. MILIONI 450 KILA MWEZI BAADA YA MITAMBO YA UMEME WA DIZELI SONGEA KUZIMWA

 Moja ya mitambo ya kufua umeme wa mafuta ya dizeli uliokuwa kwenye kituo cha Songea ikiwa imezimwa.

 NA K-VIS BLOG, SONGEA

KUTOKANA na kuzimwa kwa mitambo ya dizeli iliyokuwa ikitumika kufua umeme kwa matumizi ya mji wa Songea na vitongoji vyake Septemba 13, 2018 baada ya kuunganishwa kwenye Gridi ya Taifa, Shirika la umeme Tanzania TANESCO sasa litaokoa kiasi cha zaidi ya shilingi Milioni 450,108,508 zilizokuwa zikitumika kununua dizeli kila mwezi.


Septemba 13, 2018 TANESCO iliwasha rasmi kituo kipya na cha kisasa cha kupoza na kusambaza umeme cha Madaba, ambacho kimeunganishwa kwenye Gridi ya Taifa na hivyo kuondoa matumizi ya umeme wa mafuta kwenye Halmashauri ya Manispaa ya mji wa Songea na vitongoji vyake.


Kuwashwa kwa mtambo huo ni baada ya kukamilika kwa Mradi wa umeme wa Makambako-Songea ambao ulihusisha ujenzi wa vituo vya kupoza na kusambaza umeme vya Makambako na Songea sambamba na upanuzi wa kituo cha kupoza na kusambaza umeme cha Makambako, lakini pia Ujenzi wa njia kuu ya usafirishaji Umeme wa kilovoti 220 yenye urefu wa kilometa 245 kutoka Makambako hadi Songea kupitia Madaba. Usambazaji Umeme wa msongo wa 33kV zenye urefu wa kilomita 900 na kuunganisha wateja 22,700 katika Wilaya za Njombe , Ludewa na mji wa Makambako katika Mkoa wa Njombe, Songea Vijijini, Songea Mjini, Namtumbo na Mbinga katika Mkoa wa Ruvuma.

Tayari wakazi wa mji wa Songea wamepokea taarifa za mji wao kuunganishwa kwenye Gridi ya Taifa na hivyo kuondoa ile adha ya kukatika umeme iliyokuwa ikiwasumbua kwa muda mrefu. 

Songea kuunganishwa kwenye Gridi ya Taifa kuna maanisha mji huo sasa umeanza kupata umeme ulio bora na wa uhakika na hivyo wananchi sasa wanapaswa kuchangamkia fursa ya uwepo wa nishati hiyo kwa kufungua viwanda vidogo na miradi mbalimbali ya kiuchumi inayotegemea nishati ya umeme.
 Kituo cha Umeme TANESCO Songea ambacho kilikuwa kikitumia mashine zinazoendeshwa kwa mafuta ya dizeli. Kituo hicho sasa kimezimwa.
 Tenki la kuhifadhia mafuta ya dizeli, ambalo sasa litabaki kama kumbukumbu, baada ya matumizi yake kukoma rasmi Septemba 13, 2018.

September 1, 2018

"Tunahitaji umeme wa bei nafuu ". Dkt Kalemani

Waziri wa Nishati Dkt Medard Kalemani akifur

Waziri wa Nishati Dkt. Medard Kalemani amesema katika kuelekea uchumi wa viwanda nchi inahitaji umeme mwingi, wa uhakika, gharama nafuu na unaotabirika.

Ameyasema hayo Mkoani Njombe katika kikao kilichoshirikisha wadau mbalimbali wa ujenzi Miradi wa Maporomoko ya maji mto Rufiji (Rufiji Hydropower Project).

Alisema mradi huo ni wa miaka mingi, ulianza kubuniwa tangu Serikali ya Awamu ya kwanza mwanzoni mwa miaka ya sabini.

"Leo tunautekeleza takribani zaidi ya miaka arobaini, lakini ni kweli wakati ule mahitaji yetu ya umeme yalikuwa madogo sana na idadi ya Watanzania ilikuwa haijafika hata milioni arobaini,

"Lakini leo mahitaji yetu ya umeme ni makubwa mno na tunataka kujenga Tanzania ya Viwanda hivyo Serikali imeamua kutekeleza mradi huo", alisema Dkt. Kalemani.

Aliongeza, kwa sasa tuna umeme wa kutosha lakini hauwezi kutosheleza mahitaji ya miaka ijayo kwenye kujenga uchumi wa viwanda.

Alisisitiza kuwa, TANESCO inatakiwa kuzalisha umeme wa kutosha, wa uhakika na unaotabirika lakini pia wa bei nafuu na hivyo utekelezaji wa mradi huu ni muhimu sana.

"Potential ya maji tuliyonayo sasa hivi Tanzania ni maji ambayo yanaweza kuzalisha zaidi ya MW 4700 uwezo tulionao na ambao hatujautumia", alisema.

Aidha, Serikali itaendelea kuzalisha umeme kupitia vyanzo tofauti ikiwemo makaa ya mawe, gesi, joto radhi, upepo na mingine mingi.

Chanzo kikubwa cha maji katika mradi wa Maporomoko ya mto Rufiji ni Mto Kilombero, Ruaha Mkuu na Mto Wegwe.

Ambapo mito hiyo inapata maji kutoka vyanzo vya maji vya nyanda za juu kusini hususani maeneo ya Njombe, Makete na Waging'ombe.