February 11, 2022

MABORESHO KWENYE VISIMA VYA GESI SONGOSONGO YAKAMILIKA

 


Shirika la umeme Tanzania (TANESCO)limetangaza kukamilika kwa siku kumi za matengenezo ya mifumo katika visima vya gesi vilivyopo Songosongo jana Februari 10, 2022.

Maboresho hayo muhimu ambayo yalilenga kuongeza ujazo wa gesi ambao utakidhi mahitaji ya mitambo inayoongezwa kwenye vituo vya kuzalisha umeme vya Kinyerezi I itakayozalisha megawati 185 na Ubungo III megawati 112 na hivyo kupelekea kuongeza uzalishaji katika mfumo wa gridi kwa megawati 297.

Akitoa taarifa kwa umma leo Februari 11, 2022 Msemaji wa TANESCO, Martin Mwambene amesema kuwa Shirika hilo lilifanikiwa kutumia fursa ya matengenezo hayo kwenda sambamba na maboresho ya miundombinu ya umeme kwenye baadhi ya maeneo nchini ambayo yatasaidia huduma ya umeme kuendelea kuimarika. 

"Kutokana na mapungufu katika uzalishaji uliotokea mwaka jana kwasababu ya ukame, tuliandaa mkakati wa muda mfupi na muda mrefu na moja ya mikakati hiyo ni kuongeza uwezo wa kituo cha Kinyerezi I kutoka megawati 150 hadi 350 na kuongeza kituo cha Ubungo III kwa megawati 112" amesema Mwambene.  

Aliongeza kuwa Shirika linawashukuru wateja wake kwa uvumilivu katika kipindi chote cha siku kumi za matengenezo kilichopelekea mapungufu ya huduma ya umeme kwenye baadhi ya maeneo nchini.
  
Zoezi la matengenezo katika visima vya gesi vya Songosongo lilianza Februari 01 hadi 10, 2022 na kukamilika ndani ya wakati kama ilivyopangwa.