December 8, 2020

TANESCO yasaini mkataba wa kununua umeme kwa wazalishaji wadogo

 

Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) limeingia mkataba wa kuuziana umeme na kampuni sita binafsi ambazo zitaiuzia umeme TANESCO, Umeme ambao utaingizwa moja kwa moja kwenye kwenye gridi ya Taifa na kutumika katika maeneo mbalimbali Nchini.

Akizungumza katika hafla fupi ya kusaini mikataba kwa niaba ya Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO, Meneja Mwandamizi Uwekezaji, Mhandisi Costa Rubagumya alisema wawekezaji hao wamekidhi vigezo kwa mujibu wa kanuni zilizoidhinishwa na EWURA.

"Kwa mujibu wa kanuni zinazosimamia uendelezaji wa miradi midogo ya kuzalisha umeme, inaitaka TANESCO kuingia mikataba na wazalishaji umeme wadogo kwenye maeneo ambayo gridi ya Taifa bado haijafika", alisema Mhandisi Rubagumya.

Aliainisha vigezo vingine ni maeneo ambayo yanatatizo la umeme mdogo ili kuimarisha ubora wa umeme na kigezo kingine ni maeneo ya usambazaji umeme ambapo  njia za umeme za TANESCO ni ndefu hivyo kusababisha upotevu wa umeme.

Mhandisi Costa alizitaja kampuni hizo kuwa ni, Kahama Solar Power Project MW 10.0, Kigoma Solar Power MW 5.0, Nishati Lutheran (DKK) Investment Ltd MW 0.36.

Makampuni mengine ni, Madope Hydropower MW 1.7, Luponde Hydropower MW 0.9 na Maguta Hydropower MW 1.2.

Wakizungumza Kwa niaba ya Wazalishaji wadogo wa umeme, Padre Luciano Mpoma na Nicholas Richardson wameishukuru Serikali kupitia TANESCO kwa kukubali kufanya nao biashara ya umeme.

Waliongeza kuwa safari ilikuwa ni ndefu lakini hatimaye wamekuwa na furaha kwani lengo la Serikali ni kuhakikisha nishati ya umeme inamgusa kila mwananchi.

Makampuni hayo yanatakiwa kuanza kuiuzia TANESCO umeme ndani ya miezi 18 kuanzia leo Disemba 08,2020.

November 11, 2020

JNHPP - Zoezi la kuchepusha Maji kuanza

Kufuatia kukamilika kwa ujenzi wa handaki la kuchepusha maji katika mradi wa Julius Nyerere, kazi inayofuatia ni uchepushaji wa maji ili kuanza ujenzi wa tuta kuu.

Handaki hilo lina urefu wa mita 703 na upana wa mita 17 huku kimo chake kikiwa mita 12.

Akiongea kuhusu kufikiwa kwa hatua hiyo muhimu, Mhandisi Said Kimbanga ambaye ni Meneja Ujenzi, amesema zoezi linalofanyika kwa sasa ni utoaji wa udongo kwenye njia ya kuingilia maji, kufikia kwenye level ya 68.5 juu ya usawa wa bahari ili maji yaweze kupita.

"Hapa tulipo maji yanapita kuelekea baharini, hatuwezi kujenga tuta kuu hadi tutakapo yachepusha maji kupita kwenye handaki na eneo hilo kubaki kavu" alisema Mhandisi Kimbanga.

Aliongeza handaki hilo limekamilika kwa asilimia 100, zoezi linaloendelea ni uondoaji wa vifaa ndani ya handaki na kukata udongo uliopo mbele ya lango la kuingilia maji ili kuruhusu maji kuingia ndani ya handaki.

Aidha, zoezi lingine litakalofanyika ni ujazaji wa udongo kwenye mto kujenga tuta (cofferdam) ili kufunga mto na kuruhusu maji kupita kwenye handaki mchepusho.

Kwa upande wake Meneja Uhusiano TANESCO, Johary Kachwamba amesema kukamilika kwa mradi wa Julius Nyerere Tanzania itakuwa na umeme wa uhakika na wa gharama nafuu.

"Umeme unaozalishwa kwa maji ni umeme wa bei nafuu, kutokana na umeme wa maji kuzalishwa kwa gharama kidogo hivyo tutarajie bei ya umeme kwa Wateja kushuka" amesema Kachwamba.

Aliongeza, kutokana na umeme wa maji kuwa wa gharama nafuu ambapo unit moja inazalishwa kwa shilingi 36 TANESCO itaweza kujiendesha kwa faida zaidi.

"Tanzania inaelekea sehemu ya kihistoria, kwa kuwa na maendeleo endelevu, tutaokoa mazingira kwani wananchi wataweza kumudu gharama za umeme hivyo kuondoa matumizi ya kuni na mkaa" alisisitiza Kachwamba.
 


 
 


 

Bodi ya TANESCO yaridhishwa na uzalishaji umeme Pangani Falls


 Bodi ya Wakurugenzi TANESCO ikiongonzwa na Mwenyekiti wa Bodi Dkt. Alexander Kyaruzi imeridhishwa na utendaji kazi wa kituo cha kufua umeme cha Pangani chenye uwezo wa Mw 68.

Katika kituo hicho cha Pangani Bodi ilikagua mitambo ya kuzalisha umeme na kuridhishwa na utendaji kazi kituoni hapo. Pia bodi ilipata fursa ya kutembelea mtambo wa kuingizia maji ambayo pia yanakwenda kufua umeme kituo cha ya Hale.

Bodi ya Wakurugenzi ya TANESCO ipo katika ziara ya siku sita kutembelea na kukagua shughuli mbalimbali za TANESCO katika Mikoa ya Pwani, Tanga, Kilimanjaro na Manyara. 

 






 


October 17, 2020

KITUO CHA KUPOZA UMEME CHA DEGE KUMALIZA TATIZO LA UMEME KIGAMBONI, ILALA NA KURASINI

 

Waziri wa Nishati Dkt.Medard Kalemani  amesema kuwa mradi wa kupooza umeme wa Dege-Kigamboni jijini Dar es salaam, utaimarisha hali ya upatikanaji wa umeme katika maeneo ya Kigamboni, Kurasini na Ilala.

Akizungumza katika eneo la ujenzi wa mradi huo alipokwenda kukagua maendeleo ya ujenzi wa  mradi ,Oktoba 17, Waziri Kalemani amesema kuwa mradi huo umekamilika kwa asilimia 80 na kuitaka TANESCO kukamilisha mradi huo mapema zaidi

"Mradi huu unajengwa na TANESCO wenyewe,na wemeniambia mradi huu utakamilika Disemba mwaka huu, lakini Mimi naagiza mradi huu ukamilike mwezi ujao yaani Novemba 2020" alisema Dkt.Kalemani

Aidha, alioogezea kuwa mradi huo utaimarisha upatikanaji wa umeme kwa maeneo ya Kigamboni, Ilala na Kurasini kwa kuwa kwa sasa wanasambaziwa umeme kutoka katika  kituo kimoja Cha kupoza Umeme cha Kurasini lakini  baada ya kukamilika kwa kituo hicho, maeneo ya Kigamboni  hayatapata  shida ya umeme tena.

"Natambua kuwa kuna maeneo ya Kigamboni hayana umeme lakin niwaambie tu kuwa tatizo la umeme linakwenda kuisha kwani mara baada ya kukamilika kwa mradi huu maeneo mengi ya Kigamboni yatapata Umeme"alisema Dkt. Kalemani

Waziri pia amesema sekta ya Nishati Nchini imeimarika kwakuwa kwa  sasa Kuna vituo vya kupooza umeme 107, ambapo ndani ya miaka 5 vituo  vikubwa 43  na vituo  vidogo 7, vimejengwa ndani ya miaka mitano.

Ameongeza kwa  kusema kuwa changamoto ya kuharibika kwa miundombinu wakati wa mvua inakwenda kuisha kwani matumizi ya Nguzo za zege yameaza kutumika.

"Mradi huu umetumia Nguzo za zege, kama mnavoziona hapo nje na Nguzo hizo zimeanza kutumika maeneo yenye majimaji, ili kuepuka hali ya kukosa umeme inayotokana na Nguzo kuoza kwasababu ya maji" alisema Dkt.Kalemani.







 

September 25, 2020

"UMEME SASA NI KITONGOJI KWA KITONGOJI" DKT. KALEMANI

 


Waziri wa Nishati, Dkt. Medard Kalemani akizindua Mradi wa Ujazilizi Umeme Vijijini fungu la pili A katika Kijiji cha Bukene, Wilayani Nzega Mkoani Tabora, amesema kuwa Serikali imetenga jumla ya Shilingi bilioni 190.7 kufikisha Umeme kitongoji kwa kitongoji katika vitongoji 1,103 vya Mikoa 9.

Waziri Kalemani aliitaji Mikoa hiyo ambayo vitongoji vyake vitanufaika moja kwa moja na mradi huo kwa sasa kuwa ni, Mikoa ya Dodoma, Tabora, Kilimanjaro, Shinyanga, Mwanza, Singida, Pwani, Mbeya pamoja na Tanga.

“Uzinduzi huu wa Mradi wa Ujazilizi Fungu la pili A ni muendelezo wa usambazaji Umeme kwa Wananchi wote. Kazi hii bado inaendelea, ndani ya miaka miwili toka sasa, tutakuwa tumevifikia Vijijini vyote takriban 12,304 na Vitongoji vyake vyote 64,839 Nchini” Alisema Dkt. Kalemani

Waziri Kalemani aliendelea kwa kuwataka Watanzania ambao hawajafikiwa na huduma ya Umeme kuwa watulivu kwani lengo na mipango ya Serikali ni kuwafikishia Wananchi wote umeme ambao bado hawajafikiwa na huduma hiyo ndani ya kipindi cha miaka miwili toka sasa.

“Tumepeleka umeme kijiji kwa Kijiji na sasa tunakaribia kumaliza vijiji vyote Nchini, sasa tunakwenda kitongoji kwa kitongoji, kaya kwa kaya mpaka tutakapowafikia Wananchi wote” Alieleza Dkt. Kalemani

Kwa upande wa Wananchi wa Bukene, waliohudhuria katika uzinduzi huo walionesha kufurahishwa na kufarijika sana na mradi huo wa ujazilizi kuanzia na kuzinduliwa kitaifa katika kijiji na vitongoji vyao vya kijiji cha Bukene Migombani.

Naye Mwandu Igusule, mkazi wa eneo la Bukene, alisema kuwa wanatarajia kuutumia umeme huo kwa maendeleo yao ya kijamii pamoja na kujikwamua kiuchumi kwa kuanzisha miradi na shughuli mbalimbali zinazotegemea Nishati ya Umeme.

 






September 18, 2020

GEITA YAANZA KUNUFAIKA NA KITUO KIPYA CHA UMEM

 


 Mkoa wa Geita na maeneo ya jirani yameanza kunufaika na Mradi mkubwa wa Umeme wa Geita-Bulyanhulu baada ya kukamilika rasmi kwa mradi huo wenye laini ya kusafirisha Umeme mkubwa katika msongo wa Kilovolti 220 sambamba na Vituo viwili vya kupoza na kusambaza Umeme.

Akifanya ziara na kushuhudia uwashwaji Umeme kwa mara ya kwanza katika mradi huo, Mkuu wa Mkoa wa Geita Mhandisi Robert Gabriel, amesema kuwa, kwa muda mrefu Mkoa wa Geita ulikuwa na umeme usio tosheleza mahitaji.

“Hali iliyopelekea Serikali  kufanya jitihada za kujenga mradi huu Mkubwa ulio gharimu zaidi ya shilingi Bilioni 50 ili kuwezesha wananchi wa Mkoa wa Geita na maeneo ya jirani kupata umeme wa uhakika na gharama nafuu” alisema Mhandisi Gabriel.

Aliongeza kuwa, kukamilika kwa kituo cha kupoza umeme cha Geita hivi sasa kumewezesha Mkoa wa Geita kuwa na umeme wa uhakika utakaowezesha uwekezaji katika sekta mbali mbali hususan  uchimbaji wa Madini na Viwanda.

Mhandisi Gabriel aliwakaribisha wawekezaji kuwekeza katika Mkoa wa Geita baada ya ujio wa Umeme wa uhakika na gharama nafuu wa TANESCO.

“Hali sasa ni shwari , umeme upo wa kutosha na wa uhakika. kukamilika  kwa ujenzi wa kituo cha Geita kumewezesha mkoa kuwa na zaidi ya Megawati 85 wakati matumizi ya sasa ya  ni Megawati 16  pekee” aliongeza Mhandisi Gabriel.

Aidha, Mhandisi Gabriel amewaasa wananchi wa Mkoa wa Geita na maeneo ya jirani ambapo  miundombinu ya umeme imepita kuilinda miundombinu hiyo kwa manufaa ya kizazi hiki na kizazi kijacho. 

Mhandisi Gabriel pia ametoa onyo kuhusu tabia ya wananchi kuchoma moto mashamba kiholela, hali inayohatarisha miundombinu ya umeme. 

Aliongeza kuwa kwa mwananchi yoyote atakaye bainika kufanya uharibifu huo, hatua kali za kisheria zitachukuliwa dhidi yake ili iwe fundisho kwa wote wenye nia za namna hiyo.

Kwa upande wa TANESCO, Mhandisi Emanuel Manirabona ambaye ni Meneja Mwandamizi wa Miradi -TANESCO  amesema kuwa mradi huo wa ujenzi wa njia kubwa ya kusafirisha umeme ni miongoni mwa miradi mikubwa ya umeme inayojengwa katika Kanda ya Ziwa na Kanda ya Magharibi Kaskazini mwa Nchi.

Mhandisi Manirabona ameitaja miradi hiyo kuwa ni  njia ya umeme ya Geita-Nyakanazi yenye uwezo wa Kilovolti 220,  utakao gharimu zaidi ya shilingi Bilioni 100 pamoja na ule wa Kigoma hadi Nyakanazi msongo wa Kilovolti 400.

“yote hii ni kuhakikisha kuwa maeneo ya Uwekezaji katika Kanda ya Ziwa na Kanda ya Magharibi Kaskazini mwa Nchi yanapata umeme wa uhakika na wakutosha” Alisema Mhandisi Manirabona.

Manirabona aliongeza kuwa, kuungwa kwa njia ya kusafirisha umeme ya Bulyanhulu-Geita, kunawezesha wananchi wa mkoa wa Geita na Maeneo ya jirani na Migodi ya Bulyanhulu pamoja na Geita kuwa na umeme wa uhakika.

 







August 28, 2020

TANESCO yaunda kikosi kazi kupambana na wizi wa Umeme


 

Na Grace Kisyombe
Dar es salam.

Bodi ya Wakurugenzi  ya TANESCO imeunda kikosi kazi maalum kwa ajili ya kupambana na wizi  pamoja na hujuma katika miundombinu ya umeme.

Akizungunza katika mkutano na  Waandishi wa habari, Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi TANESCO, Dkt. Alexander L. Kyaruzi  amesema Bodi ya Wakurugenzi kupitia kamati zake imeunda kikosi kazi maalum kwa ajili ya kupambana na hujuma katika miundombinu ya umeme,

“Baadhi ya taasisi zinazoshiriki katika kampeni maalum ya kukamata wahujumu miundombinu ya umeme ni, Jeshi la Polisi, Takukuru, Ofisi ya Mwendesha mashtaka wa Serikali (DPP), Idara ya Usalama wa Taifa pamoja na wataalam wengine kutoka TANESCO na Wizara ya Nishati” Amesema Dkt. Kyaruzi

Dkt Kyaruzi aliongeza kusema kuwa, kikosi kazi hicho kitakuwa na jukumu la kukamata na kuwafikisha mahakamani wale wote wanao jihusisha na wizi pamoja na uharibifu wa miundombinu ya umeme.

Kikosi kazi hicho kimeanza kufanya kazi katika Mkoa wa Dar e salam, ambapo tayari watuhumiwa wanne wamekamatwa na kufikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu wakikabiliwa na makosa ya uhujumu uchumi.

Katika hatua nyingine Dkt. Kyaruzi amewaomba wananchi na wasamaria wema kushiriki katika kampeni hii kwa kutoa taarifa za siri ambazo zitafanikisha kuwakamata wananchi wanao hujumu miundmbinu ya umeme.

Dkt Kyaruzi amesema kuwa kutakuwa na zawadi ambazo zitakuwa zikitolewa kwa wale wote watakao fanikisha kukamatwa kwa watu wanao hujumu  miundombinu ya umeme.

Zawadi hizi ni za fedha tasilimu na kiwango cha zawadi hizi kitategemea ukubwa wa mali iliyo kamatwa au kuokolewa kutoka katika hujuma hizo.

Aidha, Dkt. Kyaruzi amewakumbusha wananchi wote wenye madeni ya umeme kulipa madeni hayo haraka kwani muda wa siku 14 ulio tolewa na Mhe Waziri wa Nishati unakaribia kwisha, hivyo basi kuanzia  Septemba 1, 2020 TANESCO itakata umeme kwa kila anaye daiwa, zoezi hili litahusu taasisi, wafanyabiashara na watu binafsi wanao daiwa.




 

August 27, 2020

Wafanyabiashara wanne wamefikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu jijini Dar es Salaam kwa uhujumu uchumi

 


Wafanyabiashara wanne wamefikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu jijini Dar es Salaam mbele ya mahakimu wawili tofauti wakikabiliwa na mashitaka ya uhujumu uchumi kwa kuingilia miundombinu ya TANESCO na kujiunganishia umeme kinyume na utaratibu.

Washitakiwa hao ni Ahmed Khalifa, mkazi wa Mikocheni, Abdulrazak Said na Anuary Amdani, ambao wote ni wakazi wa Temeke na Joseph Mwakabanga, mkazi wa Tandale kwa Tumbo,

Akisoma mashitaka hayo mbele ya Hakimu Mkuu Mkazi Kassian Matembele, upande wa mashitaka ulidai mnamo Julai 29, 2020 Mikocheni, Mtaa wa Ndovu Wilayani Kinondoni, washtakiwa kwa pamoja, Khalfan na Said waliingilia kwa makusudi miundombinu ya TANESCO.

Washtakiwa hao wanadaiwa kujiunganisha umeme kupitia mfumo wa TANESCO na kukwepa kutumia mita, kitendo ambacho ni kinyume cha sheria.

Aidha, mnamo Agosti 7, 2020 katika Mtaa wa Magomeni Mikumi Wilayani Kinondoni jijini Dar es salaam, Amdani na Mwakabanga waliingilia kwa makusudi na kinyume cha sheria miundombinu ya TANESCO iliyokusudiwa kutumiwa kusambaza huduma ya umeme.

Upande wa mashtaka ulidai kuwa washitakiwa hao walibadilisha mita, mali ya TANESCO kutoka kwenye nyumba inayomilikiwa na Amdani yenye deni ya shilingi 3,521,587.70 na kuweka mita mpya kwa lengo la kukwepa deni lililotajwa, jambo ambalo ni kinyume cha sheria.

Washtakiwa wote hawakutakiwa kujibu mashitaka yao kwa vile mashiataka yao yanaangukia kwenye sheria ya uhujumu uchumi.

Upande wa mashitaka ukiongozwa na Mawakili Waandamizi wa Serikali Mantenus Marandu and Wankyo Simon pamoja na Wakili wa Serikali Benson Mwaitenda umedai upelelezi wa mashauri yote mawili haujakamilika.

Baada ya kusomewa mashitaka yao, Mahakimu katika kesi zote mbili walitoa dhamana kwa washitakiwa kwa kuzingatia masharti mbalimbali.

Khalfan na Said walipewa masharti ya kupata wadhamani wawili kila mmoja ambaye angeweka dhamana ya shilingi milioni 5 na Kila mdhamini alitakiwa awe na barua ya utambulisho kutoka kwa mwajiri wake, kuwasilisha vitambulisho vyao, ambayo ni, kadi ya kitambulisho cha Taifa au Kadi ya kupigia kura.

Washtakiwa pia walizuiliwa kuondoka nchini bila kupata ruhusa ya Mahakama.

Kwa upande wa Amdani na Mwakabanga, hakimu aliwapa dhamana kwa masharti ya kupata wadhamini wawili kila mmoja ambaye atasaini dhamana ya 500,000 / na walitakiwa kuwasilisha vitambulisho vyao.

Kesi zote ziliahirishwa hadi Septemba 10, 2020.
 


 

Kampeni ya "PETA" yatatua kero za umeme Mkoani Tanga.

 

Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) Mkoa wa Tanga hivi karibuni limezindua Kampeni ya "PETA" lengo likiwa ni kutoa elimu ya huduma zote zitolewazo na TANESCO ikiwemo kutatua kero mbalimbali za umeme kwa wananchi.

Akizindua kampeni ya PETA Kaimu Meneja Mkoa wa Tanga Mhandisi Bakari Kalulu akiambatana na wakuu wa Idara za TANESCO Mkoa wa Tanga ili kupokea Kero za Wananchi na kuzitolea majibu yake.


Mhandisi, Kalulu alisema baadhi ya Wateja wa TANESCO wanatumia umeme kwa ajili ya kufukuza giza yaani kwa ajili ya Taa tu, PETA imekuja na majibu ya kuwahamasisha wateja waache fikra hizo na kufikiri namna nzuri ya kutumia umeme kukuza vipato vyao na Taifa kwa ujumla.

Akiielezea Kampeni hiyo, Afisa Uhusiano na Huduma kwa Wateja Mkoa wa Tanga, Bw. Amon Bandiwe alisema PETA ni kifupi cha maneno P =Pata , E =Elimu ya matumizi Bora ya umeme, T =Toa kero yako, A = Acha kuhujumu miundombinu.

Aliongeza, kampeni ya PETA itasaidia TANESCO kufikia malengo ya utoaji wa huduma ya umeme kwa Wateja na ni chachu ya kubadili fikra za Wateja kwa kutumia nishati ya umeme kukuza vipato vyao.

Kampeni hii ni suluhisho la changamoto zote za kero zinazotokana na huduma ya umeme Mkoani Tanga.

Wakazi wa Mkoa wa Tanga wameipongeza TANESCO kwa kuzindua kampeni ya PETA kampeni ambayo itaisaidia TANESCO Mkoa wa Tanga kuboresha huduma zake kwa Mkoa na Wilaya.

Aidha, Jumla ya kero 21 zilipokelewa na kujibiwa na wakuu wa Idara papo kwa papo.





 


July 18, 2020

Mradi wa Julius Nyerere hatua zote 8 zakamilika

Mafundi wakiwa wamebeba nondo wakati kazi ya ujenzi wa njia ya ardhi ya kuchepusha maji (dirvesion tunnel) ikiendelea.

HATUA zote nane (8) za utekelezaji wa ujenzi wa mradi wa bwawa la kufua umeme wa maji la Julius Nyerere (JNHPP-MW2115) kwenye bonde la mto Rufiji unaendelea kwa kasi inayohitajika, Mhandisi mkazi wa mradi huo Eng. Mushubila Kamuhabwa amewaambia waandishi wa habari kwenye eneo la mradi Julai 17, 2020.

Eng. Kamuhabwa ametaja hatua hizo kuwa ni ujenzi wa njia kubwa ya ardhini ya mchepuko wa maji (diversion tunnel), sehemu ya kufua umeme (power house), ukuta utakaotengeneza bwawa, eneo la kupokelea umeme unapozalishwa (Switch yard), power intake, barabara na madaraja, saddle dams nne na kuchakata mawe yanayotumika kutengeneza zege na mahitaji mengine.

“Mradi huu wa JNHPP una miradi mingi ndani yake na yote iko katika hatua mbalimbali na hatua hizo kama nilivyozitaja kwa pamoja ndiyo zinajenga mradi mmoja wa Julius Nyerere Hydro Power Project Megawati 2115 katika hilo ujenzi unaendelea katika maeneo yote hayo, mafundi wako kazini na wanaendelea na ujenzi kwa kasi kubwa kama inavyohitajika.” Alisema Eng. Kamuhabwa.

Alisema jambo la kufurahisha tayari mradi umeanza kuchangamsha uchumi wa nchi na kutolea mfano wakati wakiweka zege kwenye njia ya kuchepusha maji (diversion tunnel, zaidi ya tani 200 za nondo zimetumika hii inafaidisha viwanda vyetu hapa nchini lakini pia wananchi wanaokaa vijiji vinavyozunguka eneo la mradi wanafaidika kwa namna mbalimbali ikiwwemo miundombinu wezeshi kama vile umeme unaotoka Morogoro kuja hapa umepitia kwenye vijiji kadhaa natayari baadhi yao wameanza kufaidika na umeme huo.” Alisema na kuongeza…Lingine zaidi ya vijana wa Kitanzania wapatao 4,000 kutoka maeneo mbalimbali nchini hususan yale yanayozunguka eneo la mradi wameajiriwa na wanashiriki katika mradi kwa ari kubwa.

“Tunatarajia idadi hiyo ya ajira ikaongezeka hadi kufikia watu 6,000 mradi utakapofikia hatua ya juu peak.” Alisema Eng. Kamuhabwa.

Kwa upande wao baadhi ya wanakijiji wa Kisaki kilomita 60 kutoka eneo la mradi wamempongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Magufuli kwa kuwaletea mradi huo kwani tayari manufaa yake wameanza kuyaona.

“Kisaki inakuja juu, tuna uhakika mradi ukimalizika Kisaki itakuwa kama Morogoro, kwa sasa biashara inakuwa kwa kasi sana tofauti na hapo awali, mfano mchele tunauza kwa kilo shilingi 1,600/= tofauti na hapo awali tulikuwa tunauza shilingi 500/= bei ya juu kabisa shilingi 1,000/=, watu wameongezeka sana.” Alisema mwanakijiji wa Kisaki Ali Matumbo na kuongeza…umeme nao tayari umefika kijijini kwetu, shule imepata umeme kwa hivyo tunafuraha sana kwa ujio wa mradi huu na tunampongeza sana Rais wetu Magufuli.

Naye mwanakijiji mwingine Bi. Asha Said alisema, anauhakika hata barabara nzuri itajengwa kutokana na mradi huo na anafurahi kuona wageni wengi wanafika Kisaki na hivyo biashara zao zimechangamka.

Naye mwanakijiji mwingine Hassan Mohammed Ngozi alisema, anayo matumaini makubwa kwa hali anavyoiona hivi sasa hapo Kisaki, mradi utakapokamilika watakuwa na Kisaki mpya.
“Kwetu sisi ongezeko la watu hapa Kisaki limekuwa na faida kubwa………..watu wakienda kufanya kazi huko kwenye mradi wanakuja hapa kijijini wananunua bidhaa zetu na sisi tunapata pesa haya ni manufaa makubwa kwetu.” Alisema Bw. Ngozi.
Mhandisi Mkazi wa Mradi wa Julius Nyerere, Mhandisi Mushubila Kamuhabwa akizungumza na Waandishi wa Habari eneo la Mradi.

MAshine zikichoronga miamba ya ardhi ili kutengeneza njia ya kuweka baruti kwa ajili ya kulipua miamba hivyo kuhamisha milima









July 14, 2020

Utekelezaji wa Miradi ya Kimkakati



Miaka mitano imetimia Serikali  ya Awamu ya Tano ikiacha alama Sekta ya Nishati ambapo utekelezaji wa mradi Mkubwa wa kimkakati wa kufua umeme wa maji wa Julius Nyerere MW 2115 unaendelea kwa kasi.

Aidha, katika mradi wa Julius  Nyerere ujenzi wa Kituo cha Kupokea na Kusambaza Umeme (Switch yard) upo katika maandalizi ya awali ambayo ni kusafisha eneo na kufanya utafiti wa udongo yamekamilika ambayo yalianza Oktoba 2019 na Mei 2020 yamekamilika kwa kulingana na mpango kazi ulivyo.

"Utafiti wa miamba na udongo umeshafanyika pia shughuli za kusafisha eneo hilo", alisema Mhandisi Eliaza Wangwe, Mtaalamu wa miamba na udongo kwenye mradi wa Julius Nyerere.

eneo la kituo cha kupokea umeme lina ukubwa wa mita za mraba 58,075 na kituo kipo umbali wa mita 450 kutoka jengo la kuendeshea mitambo ya kufua umeme.

Zabuni ya ujenzi wa Njia Kuu ya msongo wa kilovolti 400 itakayosafirisha umeme kutoka kwenye kituo hiki kuingia kwenye gridi ya Taifa imeshatangazwa.

Aidha, utekelezaji wa maeneo mengine unaendelea na upo katika hatua mbalimbali za utekelezaji.