October 31, 2018

KATIBU MKUU NISHATI AITAKA TANESCO KUBORESHA ZAIDI UTENDAJI




Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati, Dk. Hamisi Mwinyimvua amepongeza utendaji kazi wa wafanyakazi wa Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) na kuwataka kuongeza jitihada zaidi, hususan katika ukusanyaji wa mapato.

Ameyasema hayo leo Oktoba 31, 2018 jijini Dodoma, wakati akifungua Mkutano wa 48 wa Baraza Kuu la Wafanyakazi wa TANESCO.

Akifafanua, Dk. Mwinyimvua amesema kuwa, ukusanyaji mapato unaweza kuongezeka kwa kuwaunganisha wateja wengi zaidi kadri iwezekanavyo.
“Sasa hivi mnazalisha umeme mwingi zaidi ya matumizi. Ongezeni jitihada za kuwaunganisha wateja wengi zaidi kwani ni kwa namna hiyo, mtafanikiwa kuongeza mapato ya Shirika.”

Amesema kuwa, ni matarajio ya Serikali kuona Shirika hilo linatengeneza faida kubwa itakayowezesha kutoa gawio serikalini.

Aidha, Dk. Mwinyimvua ameipongeza TANESCO kwa jitihada za kuboresha upatikanaji wa umeme lakini pia amelitaka Shirika kuongeza jitihada za makusudi kuhakikisha inazalisha umeme wa kutosha sambamba na uboreshaji wa miundombinu ya usafirishaji na usambazaji wa nishati hiyo, ili kuwezesha azma ya Taifa ya kujenga uchumi wa viwanda.

Amewataka wajumbe wa Baraza hilo, ambao wanawawakilisha wafanyakazi zaidi ya 6900 wa TANESCO nchi nzima, kujadili kwa kina namna ya kupambana na changamoto zinazolikabili Shirika ikiwemo wizi wa umeme, uharibifu wa miundombinu, ukatikaji wa umeme, ukuaji mdogo wa mapato ya Shirika, upotevu wa umeme na matatizo ya utoaji wa huduma ikiwemo uchelewaji katika kutatua matatizo ya dharura yanayowakabili wananchi.

Awali, akiwasilisha Hotuba ya Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO, Dkt. Tito Mwinuka, wakati wa Ufunguzi wa Mkutano huo; Kaimu Mkurugenzi wa Baraza la Wafanyakazi, Mhandisi Kahitwa Kashaija alisema kwamba hali ya makusanyo ya Shirika inaonesha kupanda ukilinganisha na mwaka 2017 ambapo mapato yamepanda kutoka wastani wa shilingi bilioni 146 hadi kufikia shilingi bilioni 158 kwa mwezi.

Aidha, alisema kwamba uwezo wa uzalishaji umeme umeongezeka, ambapo hadi kufikia Juni 2017 uwezo wa uzalishaji umeme kwenye gridi ulikuwa ni megawati 1263.6 wakati kwa sasa uwezo huo umeongezeka hadi kufikia takribani megawati 1600.
“Hii inajumuisha vituo nje ya gridi pamoja na wazalishaji wadogo wanaotuuzia umeme kwenye gridi na nje ya gridi.

Mkutano huo wa Baraza la Wafanyakazi TANESCO ni wa siku tatu ambapo unatarajiwa kuhitimishwa Novemba 2, mwaka huu.






September 28, 2018

Serikali inatarajia mzalishe umeme kupitia joto ardhi "Mheshimiwa Waziri Mkuu "

Waziri Mkuu wa Jamuhuri wa Muungano wa Tanzania Mhe. Majaliwa Kassim Majaliwa  akipata maelezo namna ambavyo TANESCO inawatumia watalamu wa Jiolojia katika kutekeleza miradi mbalimbali. 

NA SAMIA CHANDE, DODOMA

 Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Majaliwa Kassim Majaliwa amefungua kongamano la mwaka la Jumuiya ya Wanajiosayansi Tanzania (Tanzania Geological Society - TGS) Jijini Dodoma.

Alisema, watalamu wa Giolojia ni muhimu katika kueleta maendeleo ya Viwanda kupitia Nishati mbalimbali za umeme kama vile kuzalisha kwa kutumia Jotoardhi.

"Jotoardhi ni chanzo kizuri cha nishati kwa hivyo niwapongeze TANESCO kupitia kampuni tanzu ya TGDC, Serikali inatarajia hivi karibuni muanze kuzalisha umeme kupitia Jotoardhi", alisema Mhe. Majaliwa.

TANESCO imeshiriki katika kongamano hilo kupitia Kampuni tanzu ya Uendelezaji wa Jotoardhi Nchini (TGDC). Aidha, Mhe. Majaliwa alitembelea banda la TANESCO na kupatiwa taarifa mbalimbali kuhusu umuhimu wa Sekta ya Jiolojia katika uzalishaji, usafirishaji na usambazaji wa nishati ya umeme.

Akimuelezea Mheshimiwa Waziri Mkuu umuhimu wa jioloji katika utekelezaji wa miradi ya umeme, Mhandisi Eliaza Wangwe kutoka Idara ya Utafiti TANESCO, alisema tasnia ya jioloji ni muhimu katika utekelezaji wa miradi ya umeme katika hatua zote kuanzia utafiti, ujenzi na usimamizi. Aliongezea, TANESCO kupitia Kampuni Tanzu TGDC inaendelea kufanya tafiti mbalimbali ili kuwezasha uzalisha umeme utokanao na rasilimali ya jotoardhi.
"Jotoardhi ni nishati jadidifu, nafuu na endelevu inayoweza kutumika katika kuzalisha umeme na matumizi mengine kama vile kilimo, ukaushaji wa mazao na ufugaji wa samaki", alisema Mhandisi Wangwe.

 Kwa upande wake Meneja Mipango na Miradi kutoka TGDC Mhandisi Shakiru Kajugus, alisema Tanzania ina uwezo wa kuzalisha zaidi ya Megawati 5000 zitokanazo na jotoardhi.

 “Nchi yetu ina zaidi ya maeneo 50 yenye viashiria vya Jotoardhi ambapo maeneo hayo mengi yanapatikana katika Bonde la Ufa la Afrika Mashariki ambalo linapita hadi Kenya ambao tayari wanazalisha zaidi ya 700MW za Jotoardhi kwa sasa.” Mhandisi Kajugus.

 TGDC inaendelea na tafiti katika maeneo mbalimbali nchini kama vile eneo la Ziwa Ngozi lililoko Mkoani Mbeya ambapo ndipo yalipo makutano ya bonde la ufa la upande wa mashariki na lile la magharibi. Utafiti huo katika hatua ya uchorongaji visima vya majaribio ili kuthibitisha uwepo na kiwango cha rasilimali ya jotoardhi iliyopo katika eneo hilo.

Katika kukuza uchumi wa viwanda joto ardhi itatumika katika miradi mbalimbali kama kilimo na viwandani.




September 15, 2018

TANESCO KUOKOA ZAIDI YA SH. MILIONI 450 KILA MWEZI BAADA YA MITAMBO YA UMEME WA DIZELI SONGEA KUZIMWA

 Moja ya mitambo ya kufua umeme wa mafuta ya dizeli uliokuwa kwenye kituo cha Songea ikiwa imezimwa.

 NA K-VIS BLOG, SONGEA

KUTOKANA na kuzimwa kwa mitambo ya dizeli iliyokuwa ikitumika kufua umeme kwa matumizi ya mji wa Songea na vitongoji vyake Septemba 13, 2018 baada ya kuunganishwa kwenye Gridi ya Taifa, Shirika la umeme Tanzania TANESCO sasa litaokoa kiasi cha zaidi ya shilingi Milioni 450,108,508 zilizokuwa zikitumika kununua dizeli kila mwezi.


Septemba 13, 2018 TANESCO iliwasha rasmi kituo kipya na cha kisasa cha kupoza na kusambaza umeme cha Madaba, ambacho kimeunganishwa kwenye Gridi ya Taifa na hivyo kuondoa matumizi ya umeme wa mafuta kwenye Halmashauri ya Manispaa ya mji wa Songea na vitongoji vyake.


Kuwashwa kwa mtambo huo ni baada ya kukamilika kwa Mradi wa umeme wa Makambako-Songea ambao ulihusisha ujenzi wa vituo vya kupoza na kusambaza umeme vya Makambako na Songea sambamba na upanuzi wa kituo cha kupoza na kusambaza umeme cha Makambako, lakini pia Ujenzi wa njia kuu ya usafirishaji Umeme wa kilovoti 220 yenye urefu wa kilometa 245 kutoka Makambako hadi Songea kupitia Madaba. Usambazaji Umeme wa msongo wa 33kV zenye urefu wa kilomita 900 na kuunganisha wateja 22,700 katika Wilaya za Njombe , Ludewa na mji wa Makambako katika Mkoa wa Njombe, Songea Vijijini, Songea Mjini, Namtumbo na Mbinga katika Mkoa wa Ruvuma.

Tayari wakazi wa mji wa Songea wamepokea taarifa za mji wao kuunganishwa kwenye Gridi ya Taifa na hivyo kuondoa ile adha ya kukatika umeme iliyokuwa ikiwasumbua kwa muda mrefu. 

Songea kuunganishwa kwenye Gridi ya Taifa kuna maanisha mji huo sasa umeanza kupata umeme ulio bora na wa uhakika na hivyo wananchi sasa wanapaswa kuchangamkia fursa ya uwepo wa nishati hiyo kwa kufungua viwanda vidogo na miradi mbalimbali ya kiuchumi inayotegemea nishati ya umeme.
 Kituo cha Umeme TANESCO Songea ambacho kilikuwa kikitumia mashine zinazoendeshwa kwa mafuta ya dizeli. Kituo hicho sasa kimezimwa.
 Tenki la kuhifadhia mafuta ya dizeli, ambalo sasa litabaki kama kumbukumbu, baada ya matumizi yake kukoma rasmi Septemba 13, 2018.

September 1, 2018

"Tunahitaji umeme wa bei nafuu ". Dkt Kalemani

Waziri wa Nishati Dkt Medard Kalemani akifur

Waziri wa Nishati Dkt. Medard Kalemani amesema katika kuelekea uchumi wa viwanda nchi inahitaji umeme mwingi, wa uhakika, gharama nafuu na unaotabirika.

Ameyasema hayo Mkoani Njombe katika kikao kilichoshirikisha wadau mbalimbali wa ujenzi Miradi wa Maporomoko ya maji mto Rufiji (Rufiji Hydropower Project).

Alisema mradi huo ni wa miaka mingi, ulianza kubuniwa tangu Serikali ya Awamu ya kwanza mwanzoni mwa miaka ya sabini.

"Leo tunautekeleza takribani zaidi ya miaka arobaini, lakini ni kweli wakati ule mahitaji yetu ya umeme yalikuwa madogo sana na idadi ya Watanzania ilikuwa haijafika hata milioni arobaini,

"Lakini leo mahitaji yetu ya umeme ni makubwa mno na tunataka kujenga Tanzania ya Viwanda hivyo Serikali imeamua kutekeleza mradi huo", alisema Dkt. Kalemani.

Aliongeza, kwa sasa tuna umeme wa kutosha lakini hauwezi kutosheleza mahitaji ya miaka ijayo kwenye kujenga uchumi wa viwanda.

Alisisitiza kuwa, TANESCO inatakiwa kuzalisha umeme wa kutosha, wa uhakika na unaotabirika lakini pia wa bei nafuu na hivyo utekelezaji wa mradi huu ni muhimu sana.

"Potential ya maji tuliyonayo sasa hivi Tanzania ni maji ambayo yanaweza kuzalisha zaidi ya MW 4700 uwezo tulionao na ambao hatujautumia", alisema.

Aidha, Serikali itaendelea kuzalisha umeme kupitia vyanzo tofauti ikiwemo makaa ya mawe, gesi, joto radhi, upepo na mingine mingi.

Chanzo kikubwa cha maji katika mradi wa Maporomoko ya mto Rufiji ni Mto Kilombero, Ruaha Mkuu na Mto Wegwe.

Ambapo mito hiyo inapata maji kutoka vyanzo vya maji vya nyanda za juu kusini hususani maeneo ya Njombe, Makete na Waging'ombe.








August 28, 2018

TANESCO YAZALISHA UMEME WA KUTOSHA


Imebainishwa kuwa Shirika la Umeme la Tanzania (TANESCO) kwa sasa linazalisha umeme wa kutosha mahitaji ya nchi huku ziada ikiwa ni zaidi ya megawati 200 na hivyo kupelekea kupungua kwa changamoto ya kukatika umeme mara kwa mara.

Hayo yamesemwa na Mkurugenzi  Mtendaji wa TANESCO,  Dkt. Tito Mwinuka,  leo tarehe 28/08/2018 wakati akiwasilisha Taarifa ya Shirika hilo kwa Kamati  ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini.

Ameeleza kuwa, umeme unaozalishwa sasa ni takribani megawati 1517.47 huku matumizi yakiwa ni takribani ni megawati 900.

Aidha, Dkt. Mwinuka ameeleza kuwa Shirika hilo linaendelea na juhudi za kuwaunganishia umeme wananchi, kazi ambayo inaenda  sambamba na kuimarisha mifumo ya usafirishaji na usambazaji wa umeme ili kupunguza  matukio ya kukatika kwa umeme mara kwa mara.

Ameeleza kuwa, kutokana na jitihada hizo, mapato ya Shirika yamekuwa yakiongezeka mwaka hadi mwaka na kuliwezesha Shirika kujiendesha bila kutegemea ruzuku kutoka serikalini tangu mwaka 2015/16.

“Mapato ya Shirika yameendelea kuimarika ambapo katika kipindi cha mwaka 2017/18, makusanyo yamekuwa ya wastani wa  shilingi bilioni 38 hadi 39 kwa Wiki kutoka wastani wa shilingi bilioni  34 katika mwezi Aprili, 2018,” amesema Dkt. Tito Mwinuka.

Akizungumzia suala la deni la TANESCO, Dkt. Mwinuka amesema kuwa  kuna sababu mbalimbali zinazopelekea deni la Shirika kuongezeka ikiwa ni pamoja na gharama kubwa za uzalishaji wa umeme katika maeneo yaliyopo mbali na gridi ya Taifa ambapo TANESCO hulazimika kuzalisha umeme kwa wastani wa shilingi 763 kwa uniti moja.

Akizungumzia mikakati ya Shirika katika kulipa madeni kwa wadai wake, Dkt.  Mwinuka alisema kuwa wameweka mipango mahsusi ili kulipa gharama hizo kila mwezi ili deni lisiendelee kukua, kuwalipa deni lote wadai wadogowadogo kwa wakati na kujadiliana na wadai ili kuondoa riba.

Aliongeza kuwa,  juhudi nyingine zinazofanywa na TANESCO ili kupunguza madeni kwa Shirika ni  kutafuta mikopo yenye masharti nafuu,  kuongeza na mapato.


August 17, 2018

Kamanda wa Polisi kanda maalum ya Dar es Salaam Lazaro Mambosasa akizungumza na waandishi wa habari kutangaza operesheni maalum ya wahalifu wa miundombinu ya umeme na maji.


Kamanda wa Polisi kanda maalum ya Dar es Salaam Lazaro Mambosasa akizungumza na waandishi wa habari kutangaza operesheni maalum ya wahalifu wa miundombinu ya umeme na maji.
Dar es salaam.

Jeshi la Polisi Kanda Maalum ya Dar es salaam limezindua operesheni itakayowezesha kutokomeza wanaohujumu miundombinu ya maji na umeme.

Operesheni hiyo imezinduliwa leo Agosti 17, 2018 na Kamanda wa polisi Kanda Maalum Lazaro Mambosasa alipokutana na wadau kutoka shirika la umeme (TANESCO) pamoja na shirika la maji safi (DAWASCO)

Kamanda Mambosasa amesema siku zahivi karibuni kumekuwa na wimbi kubwa la watu wanaojiunganishia miundombinu hiyo bila kufuata utaratibu na kuzisababishia hasara kampuni hizo

Kaimu Meneja uhusiano wa Tanesco Leila Muhaji amesema watashirikiana na jeshi la polisi kuhakikisha wote wanaohujumu miundombinu hiyo wanakamatwa.

 “Tutashirikiana na jeshi la polisi Kanda maalum kuhakikisha wote wanaohujumun miundombinu hii tunawakamata kwakuwa wamekuwa wakiliingizia shirika hasara hasa wanapoiba mafuta kwenye transfoma kwaajili ya kupikia”amesema Muhaji.

Ameongeza kuwa kwa sasa umeme unapatikana kwa urahisi kwenye maeneo yote na shirika linaende kusambaza umeme kwenye maeneo ambayo haujafika.

August 16, 2018

Waziri kalemani awasha rasmi umeme katika Mahakama ya mwanzo ya Somanda

Waziri wa Nishati, Dkt. Medard Kalema akikata utepe.

Mahakama ya mwanzo ya Somanda
Waziri wa Nishati, Dkt. Medard Kalemani amewasha rasmi umeme katika Mahakama ya Mwanzo ya Somanda Wilayani Bariadi Mkoa wa Simiyu kupitia Mradi wa Umeme Vijijini Awamu ya Tatu (REA 111).

Waziri Kalemani amefanya uzinduzi huo jana, Agosti 15, 2018 katika eneo la Mahakama ya Mwanzo ya Somanda mkoani Simiyu akiwa katika ziara yake katika Kanda ya Ziwa.

Waziri Kalemani alieleza kuwa ni faraja kwake kuona taasisi za umma zikiwemo Mahakama zikipata umeme.

“Mahakama nyingi zilikuwa hazina umeme, na hii ni mojawapo ya changamoto ambayo inapekea kesi nyingi mahakama kuchelewa, hivyo Mahakama ya Somanda mtaharakisha kutoa hukumu ya kesi ili kutenda haki kwa wananchi” alisema Waziri Kalemani.

Waziri Kalemani alisema kuwa, kipaumbele cha Serikali ni kupeleka nishati ya umeme katika Taasisi zote za umeme ili kuwafikia wananchi wengi kwa wakati moja.

Akizungumza katika mkutano huo, Waziri Kalemani alisema kuwa sasa mahakama ya Somanda watafanya kazi zao muda wowote na pia wanaweza kuweka vinasa sauti ili kupata ushahidi wa uhakika kutoka kwa mashahidi wao.

Aidha, Waziri Kalemani alikumbusha Mahakama hiyo kulipia bili zao za umeme kwa wakati ili kuepuka kukatiwa umeme na kusababisha usumbufu kwa wananchi.
Pia, Waziri Kalemani aliagiza Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) kuweka Transforma moja katika mahakama hiyo special kwao wao wenyewe ili kuepuka usumbufu wowote utakaojitokeza kama vile kukatika kwa umeme.

“Wekeni Transfoma ya Mahakama hii wao peke yake ili ikitokea umeme umekatika maeneo mengine wao wasipate usumbufu ili wafanye kazi yao kwa ufanisi,”alisema Waziri Kalemani.

Waziri Kalemani pia, alikabizi vifaa cha Umeme Tayari (UMETA) 20 kwa Mahakama hiyo lengo likiwa ni kuhamasisha matumizi ya vifaa hivyo vya UMETA katika Taasisi za umma ambavyo havihitaji gharama kubwa kuviunganisha na vinawasha vyuma viwili hadi vinne.


Waziri wa Nishati, Dkt. Medard Kalemani (wa tatu kulia) akishangilia mara baada ya kukata utepe ikiwa ni ishara ya kuwasha rasmi umeme katika Mahakama hiyo. Wa pili kulia ni Mkuu wa Mkoa wa Simiyu Antony Mktaka na wa tano kulia ni Hakimu wa Mahakama ya Mwanzo David Peter.


Waziri wa Nishati, Dkt. Medard Kalemani( katikati kwa waliokaa) akiwa katika picha ya pamoja mara bada ya kuwasha umeme rasmi katika Mahaka ya Mwanzo ya Somanda wilayani Bariadi. Wengine katika picha ni Wafanyakazi kutoka Serekalini.



August 2, 2018

Rufiji Hydropower Project MW 2100 kuendesha treni ya umeme

Wazi Waziri wa Nishati Dkt. Medard Kalemani akifungua kikao hicho, kushoto ni Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, William Lukuvi ma kulia ni Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), January Makamba 

MOROGORO 

WAZIRI wa Nishati, Dk. Medard Kalemani, amesema kuwa umeme utakaozalishwa kwenye mradi wa Rufiji Hydropower Project  (Strigler’s Gorge)ndio utakaotumika katika uendeshaji wa treni ya kisasa ya umeme.

Kutokana na hali hiyo amesema kuwa Serikali itakikisha inasimamia kikamilifu utekelezaji wa mradi huo kwa wakati ili uweze kuleta manufaa kwa wananchi na Taifa kwa ujumla.

Hayo aliyasema jana mjini Morogoro, alipokuwa akifungua kikao cha mawaziri, makatibu wakuu wa wizara na wataalamu mbalimbali zikiwamo Wizara 11 ambao wanatekeleza mradi huo.

Alisema mradi huo pindi utakapokamilika unatarajiwa kuzaliwa megawati 2,100 pindi utakapokamilika mwaka 2010.

 “Hivyo tumekutana hapa kujadili taarifa ya wataalamu kuhusu mradi, kutafakari changamoto na kuzifanyia kazi pamoja na kutembelea eneo la mradi.

“Hivi pamoja na hali hiyo kutakuwa na kazi ya kujenga transmi,” alisema Dk. Kalemani.
Kutokana na umuhimu mkubwa wa mradi huo kwa Taifa, Dk. Kalemani, alisema Serikali itachukua hatua za kisheria kwa yeyote atakayekwamisha uwetekelezaji wa mradi huo ambao utekelezaji wake unahusisha wizara 11 huku ukisimamiwa na Wizara ya Nishati kupitia Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco).

Waziri huyo wa Nishati, alisema tangu ilipoasisiwa azma ya utekelezaji wa mradi huo na Rais Dk. John Magufuli, Julai mwaka jana Serikali kupitia Wizara ya Nishati kwa kushirikiana na wizara nyingine walianza usimamizi wa haraka wa utekelezaji wake.
“Mradi huu utazalisha Megawati 2,100 ulibuniwa miaka mingi lakini ulichelewa kutekelezwa. Julai mwaka uliopita (2017) Rais Dk. John Magufuli aliweka wazi azma ya utekelezaji wa mradi huu.

“Waheshimiwa mawaziri na wajumbe mradi wa Mto Rufiji unaweza kuusema ni mradi rahisi sana kama miradi mingine lakini kwa historia ya uzalishaji wa umeme kwa nchi yetu huu utakuwa mradi mkubwa sana.

“Mradi mkubwa tuliona kwa sasa wenye megawati nyingi 240, ambao ni Kinyerezi namba mbili na katika miradi ya miradi ya maji ni wa megawati 204 kwa hiyo kuna kila namna ya kuongeza juhudi za kuukamilisha mradi huu. Nichukue nafasi hii kwa heshima kubwa kuipongeza Serikali hasa kupitia kwa Mheshimiwa Rais kwa kuamua kuutekeleza mradi huu nasi kama wasimamizi na watekelezaji wake tutatumia kila namna kila nguvu na akili tuliyonayo kuutekeleza kwa dhati mradi huu hadi ukamilike.

“Hatutasita kuchukua hatua kwa mtu yeyote mwenye nia ama ya kuuchelewesha ama kuukwamisha hatutasita kuchukua hatua za kisheria sisi tunaomba mradi huu ndio mkombozi pekee. Kama Serikali tumedhamiria kuutekeleza mradi huu na tumejipanga vizuri,” alisema
Alisema jambo la kwanza linalohitajika ni spidi ya utekelezaji kwa wataalamu na usahihi wa utekeleza wake pamoja na uweledi kwenye mradi huo.

Waziri huyo wa Nishati alisema
Alisema kwa sasa Serikali inaendelea kumtafuta mkandarasi ambaye atatekeleza mradi huo pamoja na msimamizi wa mkandarasi ambaye sharti apatikane kabla mkandaasi hajapatikana.

“Tunaendelea kutekeleza miradi ya kujenga miradi ya kujenga usafirishaji wa umeme huo (trasmision line)  ya kuutoa umeme huo Rufiji na kuupeleka hadi Chalinze ambapo umeme huu pia unautarajia sana utumike kuendesha treni mpya ya Standard Gauge inayoanza kutumika mara baada ya mradi kukamilika.

“Kwa hiyo huu ni mradi muhimu kwetu sisi Serikali maandalizi yanakwenda sawa ikiwamo kuanza kuona kuona kuanzia sasa namna ya utekelezaji wake,” alisema Dk. Kalemani

Kama mtakumbuka Bonde la Rufiji lilikuwa chini ya usimamizi wa RUBADA, lakini kwa kuwa wao walikuwa wakisimamia walishindwa kuutekeleza kutokana na kuwa wao si kazi yao kujenga umeme kwani lilikuwa jukumu la Tanesco.

“Mwaka jana tulipoanza mradi kuliwapo na changamoto za kawaida ikiwamo kujenga uelewa wa mradi huu. Hivyo ninapenda kusema kwamba taratibu za kumpata mkandarasi zinaendelea na kufikia Septemba mwaka huu atakuwa amepatikana. Kazi yetu sisi ni kuweka mazingira wezeshi kwa mkandarasi ili awezwe kuutekeleza mradi huu kwa wakati,” alisema Dk. Kalemani
Alisema lengo la mkutano huo utaangalia masuala matatu ambayo ni kupata taarifa ya utekelezaji na hatua za kuchukua, kutafakari changamoto za mradi na kutembelea eneo la mradi ili kuona hali halisi.

Dk. Kalemani, alisema ni vema kila mtaalamu kwa nafasi hasa waliohudhuria kwenye mkutano huo kutafakari kwa kina na hatua za kuchukua ili kuhakikisha utekelezaji unakamilika kwa wakati.
Alisema kwa sasa nchi ina Megawati 1582 baada ya kuongezewa uwezo wa mtambo wa umeme wa Kinyerezi II na mwishoni mwakani zitaingizwa megawati 185 kupitia mtambo wa Kinyerezi I.

“Lengo ni kufikisha megawati 500 hadi kufikia mwaka 2020 na ifikapo mwaka 2025 kuwa na megawati 10,000. Mradi huu tunaweza kusema ni rahisi lakini pia ni wa kihistoria na ndiyo mradi mkubwa kwetu. Na tutaukamilisha kama ulivyopangwa na serikali.

“kupitia mkutano huu utapata taarifa na mazingira wezeshi kwa kila mdau ili kuweza kuona wapi kuna changamoto na namna ya kuchukua ili twende haraka,” alisema

Waziri huyo wa Nishati, alisema kuwa kikao hicho cha mawaziri ni cha pili kufanyika ambapo cha kwanza kilifanyika Aprili mwaka huu.


Mkutano huu umehudhuriwa na Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, William Lukuvi, Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), January Makamba pamoja na makatibu wakuu wa Wizara Malisili na Utalii, Ofisi ya Makamu wa Muungano na Mazingira, Wizara ya Kilimo, Wizara ya Ujenzi na Wizara ya Uchukuzi.






July 30, 2018

Singida yanufaika na Miradi ya Umeme Vijijini (REA)


Afisa Uhusiano na Huduma kwa Wateja Mkoa wa Singida Witness Msumba akiwaelewesha Wananchi wa Kijiji cha Marya juu ya kifaa cha UMETA ambacho ni mbadala wa "Wiring" ndani kwenye nyumba ndogo.


Na Grace Kisyombe - Singida

Shirika la umeme Tanzania (TANESCO)  limeendelea na utoaji elimu kwa umma kuhusu  miradi ya umeme vijijini,
Akizungumzia miradi inayoendelea mkoani Singida Mhandisi Abrahmani Nyenye  ambaye ni Meneja wa TANESCO   Mkoa  wa Singida amesema, "Mkoa wa Singida una jumla ya Wateja 34, 185   ujio wa miradi ya umeme vijijini itaongeza wateja 8648 itakapo kamilika" Ambapo aliitaja miradi iliyopo ni Mradi wa uunganishaji umeme vijijini kupitia ufadhili wa Mradi wa njia ya usafirishaji umeme ya 400kV utokao Iringa hadi shinyanga (BTIP )ambao utawanufaisha wanavijiji walio pitiwa na njia hiyo ya umeme ambapo kwa mkoa wa Singida ni vijiji 39 vitanufaika na mradi huu wa BTIP .

Mradi wa pili ni ule wa REA awamu ya Pili  ambao ulipaswa uwe umekamilika lakini kwa changamoto mbali mbali mradi huu bado unaendelea katika baadhi ya vijiji vya Mkoa wa Singida ,

Mradi wa tatu ni ule wa REA awamu ya Tatu ambao umeanza mnamo mwezi wa tano na utakuwa na awamu tatu zinazo tarajiwa kukamilika mnamo mwaka 2021. Akiendelea kuzungumzia miradi hii Mhandisi Nyenye alisema hadi kukamilika kwa miradi yote mitatu Jumla ya vijiji 156 vitakuwa vimepatiwa umeme.

Akihamasisha uwekezaji mhandisi Nyenye alisema Kuna maeneo ya uwekezaji kama eneo la uchimbaji dhahabu la Sekenke tayari limesha patiwa umeme kwa wawekezaji wawili , na kwa kupitia miradi hii wawekezaji ( wachimbaji wadogowadogo ) wa dhahabu pia watapatiwa huduma ya umeme kuanzia vitalu vya Sekenke 1 hadi Sekenke 5 wachimbaji wote watapatiwa umeme.
Pamoja na kuhamasisha uwekezaji Mhandisi Nyeye aliwaasa wanavijiji kulinda miundombinu ya umeme kwani Serikali imewekeza fedha nyingi katika miradi hii hivyo ni vema wanachi wakalinda miundo mbinu hiyo.

 Akitolea mfano eneo la Sekenke ambapo baadhi ya wananchi walianzisha machimbo katika eneo zilipo nguzo za umeme mkubwa wa 400kV , Mhandisi Nyenye alionya kuhusu kuto kufanya shughuli zozote za kibinadamu  katika njia hizo za umeme kwani ni hatari kwa maisha yao pamoja na hasara kwa Serikali kwani endapo itatokea nguzo hizo zikaanguka .

Naye bi Adelina Lyakurwa ambaye ni afisa Masoko kutoka TANESCO makao makuu, aliwahamasisha wananchi kuhusu kuchangamkia fursa hii ambapo kila mwananchi aliye katika miradi hii yote mitatu afuate taratibu za kuunganishiwa umeme kwani katika muda wa mradi mteja atalipia tshs 27,000 tu ili apatiwe huduma. Gharama ambayo ni kodi ya ongezeko la.thamani pekee.

Meneja wa TANESCO Mkoa wa Singida Mhandisi Abrahaman M.A Nyenye akitoa taarifa ya utekelezaji Miradi ya Umeme Mkoani kwake.





July 15, 2018

"TANESCO Changamkieni fursa" Naibu Waziri Nishati


Naibu Waziri wa Nishati, Subira Mgalu akizungumza na wananchi wa Kijiji cha Iputi, Kata ya Mbuga, Wilayani Ulanga, akiwa katika ziara ya kazi Mkoani Morogoro,


Na Veronica Simba – Ulanga

Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Subira Mgalu amewataka watendaji wa Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) kuwa wabunifu na kuzitumia vema fursa za kibiashara zinazojitokeza kwa kupeleka umeme katika maeneo mbalimbali yenye Wateja wengi wanaohitaji huduma hiyo.

Alitoa agizo hilo akiwa katika ziara ya kazi kwenye maeneo mbalimbali ya Wilaya ya Ulanga, Mkoani Morogoro.

Naibu Waziri alisisitizia kauli yake hiyo na kuwaagiza Meneja wa Kanda na Mkoa, kuandaa Mradi mdogo unaolenga kuwapelekea umeme Wananchi wa eneo hilo mapema iwezekanavyo, kabla hawajafikiwa na Mradi wa Ujazilizi.

“Nawaachia kazi hii, muandae Mradi wa kuwaletea Wananchi hawa umeme. Nimeona uwezo wa kulipa wanao na wamesubiri kwa muda mrefu sana. Wako tayari.” Alisema Mhe. Mgalu.

Kabla ya kutoa agizo hilo, Mhe. Mgalu  aliwauliza Wananchi ikiwa wako tayari kupelekewa huduma hiyo na TANESCO kwa gharama ya shilingi 177,000 au wasubiri Mradi wa Umeme Vijijini Awamu ya Tatu, Mzunguko wa Kwanza (REA IIIA) uwafikie ambao utawagharimu shilingi 27,000 tu; na kwa umoja wao walitaka wapelekewe umeme wa TANESCO kwa madai kuwa wanao uwezo wa kulipia.

Aidha, alikiri kukerwa na utendaji kazi duni uliooneshwa na Mkandarasi MBH, aliyekuwa akitekeleza Mradi wa Umeme Vijijini Awamu ya Pili (REA II) katika Mikoa ya Pwani na Morogoro; ambapo alieleza kwamba ndiyo sababu Serikali haijampatia tena kazi.

Kufuatia suala hilo, aliwaagiza watendaji wa TANESCO, kuandaa taarifa ya utekelezaji wa Mradi huo na kuiwasilisha ofisini kwake Dodoma, kabla ya Ijumaa ijayo, Julai 20 mwaka huu.

“Natambua kuwa Mkandarasi husika alikwishalipwa lakini zipo fedha kidogo zilizosalia kukamilisha malipo yake. Tutafute utaratibu utakaowezesha kuhamishia fedha hizo TANESCO ili zisaidie kutekeleza Mradi wa Ujazilizi badala ya kumlipa mtu ambaye ametutia hasara kwa utendaji duni,” alisisitiza.

Pia, alitoa onyo kwa Wakandarasi wanaotekeleza Miradi mbalimbali ya Umeme Vijijini, hususan REA III, kuwa Serikali haitamvumilia yeyote atakayeharibu kazi kwa namna yoyote.
Aidha, sambamba na onyo hilo, alisema kuwa, Serikali itamuwajibisha pia Msimamizi wa Serikali wa Mradi husika, ambaye atabainika kushindwa kumsimamia ipasavyo Mkandarasi na kusababisha kutotekelezwa kwa Mradi kikamilifu.

Maelekezo mengine aliyoyatoa Naibu Waziri katika ziara hiyo, ni kwa TANESCO na Wakala wa Nishati Vijijini (REA), kuhakikisha wanaunganisha umeme katika maeneo yote yaliyopitiwa na miundombinu ya umeme.

Akifafanua zaidi, alisema kuwa, Serikali ya Awamu ya Tano haitaki kuona wananchi ambao wamepitiwa na miundombinu ya umeme, wakiishia kuangalia tu nyaya na nguzo pamoja na kuzilinda huku wao wenyewe wakiwa hawana umeme.
“Hili ni agizo kutoka kwa viongozi wetu wa juu, wakiongozwa na Mheshimiwa Rais John Magufuli, hivyo kilichobaki ni utekelezaji wake.”

Naibu Waziri amekuwa katika ziara ya kazi kwa takribani wiki tatu, katika Mikoa mbalimbali nchini, kukagua utekelezaji wa Miradi mbalimbali ya umeme pamoja na kuzungumza na wananchi. Vijiji vingine alivyotembelea wilayani Ulanga, ambako ndiko amehitimisha ziara yake, ni pamoja na Chikwera, Kata ya Mwaya pamoja na Kijiji cha Makanga, Kata ya Vigoi.

Baadhi ya watendaji kutoka Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) na Wakala wa Nishati Vijijini (REA), wakimsikiliza Naibu Waziri wa Nishati, Subira Mgalu (hayupo pichani), alipokuwa akizungumza na wananchi wa Kijiji cha Makanga, Kata ya Vigoi, Wilaya ya Ulanga, Ijumaa Julai 13, 2018 akiwa katika ziara ya kazi.

Mbunge wa Ulanga, Goodluck Mlinga, akizungumza wakati wa ziara ya Naibu Waziri wa Nishati, Subira Mgalu (wa pili kutoka kulia), Kijiji cha Makanga, Kata ya Vigoi, wilayani Ulanga, Ijumaa Julai 13, 2018 kukagua utekelezaji wa miradi ya umeme.

Sehemu ya umati wa wananchi wa Ulanga, mkoani Morogoro, wakimsiliza Naibu Waziri wa Nishati, Subira Mgalu (hayupo pichani), alipowatembelea Ijumaa, Julai 13 mwaka huu, akiwa katika ziara ya kazi na kuwaeleza mikakati ya Serikali kuwapelekea umeme wa uhakika.


July 12, 2018

Dkt. Kalemani ameendelea na uzinduzi Miradi ya Umeme Vijijini Mkoani Tabora


Waziri wa Nishati Dkt. Medard Kalemani, ameendelea na ziara ya uzinduzi wa Miradi ya Umeme Vijijini Awamu ya Tatu katika Wilaya za Kaliua, Sikonge na Uyui Mkoani Tabora.

Dkt. Kalemani amezindua katika Vijiji vya Ghuliyankulu, Mbeta, Uyowa, Mkindo na Mwongozo vilivyopo Wilaya ya Kaliua.

Vijiji vingine ni Kisanga na Kanyamsenga katika Wilaya ya Sikonge.

Mheshimiwa Waziri ataendelea na ziara kesho ambapo anatarajiwa kutembelea kijiji cha Mbuyuni kilichopo Wilaya ya Uyui.


July 11, 2018

Dkt. Medard Kalemani azindua Mradi wa Umeme Vijijini Awamu ya III Wilayani Kasulu Mkoani Kigoma



Waziri wa Nishati Dk. Medard Kalemani, akiambatana na  Viongozi wengine wa Serikali Wilayani Kasulu na Mkoa kigoma, amezindua mradi wa umeme Vijijini Awamu ya Tatu kwa Vijiji 149 vya Mkoa wa Kigoma.

Kwa Mkoa wa Kigoma uzinduzi huo umefanyika katika Kijiji cha Rusesa Wilayani Kasulu.

Katika uzinduzi huo Dkt. Kalemani alitoa maagizo kwa wasimamizi wa mradi huo kwa Wilaya nne ambazo zilichelewa kupata mradi huo na kuwataka wasimamizi TANESCO na Wakala wa Nishati Vijijini kuhakikisha wanamsimamia Mkandarasi ili ifikapo mwezi Juni, 2019 mradi uwe umekamilika.

Aidha, alitoa maagizo kwa Uongozi wa TANESCO Mkoa wa Kigoma kuanzisha Ofisi ndogo katika eneo la Rusesa kwa minajili ya kusikiliza kero za Wateja na kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora na kwa gharama zilizoidhinishwa na Serikali.

Pia Dkt. Kalemani aliwasisitiza Wananchi kuhakikisha wanalinda miundombinu ya umeme kwani inagharimu pesa nyingi kujengwa"Niwaombe Wananchi muitunze miundombinu itakayojengwa kwa kuwa Serikali imetumia gharama kubwa sana kuwekeza katika miradi ya umeme". Alisisitiza.

Awali, akimkaribisha Mheshimiwa Waziri kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Kigoma, Mkuu wa Wilaya ya Buhingwe na ambaye pia anakaimu Wilaya ya Kasulu Brigedia Jenerali Marco Gaguti alisemaWananchi wamekuwa wakiulizia kupatiwa huduma ya umeme mara kwa mara "Naamini uzinduzi huu utakuwa chachu kwa Wananchi kuanzisha Viwandavikubwa, vidogo na vya kati".






TANESCO Rukwa, NMB watembelea Gereza la Molo

Wafanyakazi wa Shirika la Usambazaji umeme ( TANESCO) Mkoa wa Rukwa wakishirikiana na Benki ya NMB wamewatembelea Maafisa wa Magereza wa Gereza la Molo lililopo Mkoani Rukwa na kutoa elimu inayohusu taratibu za kuunganishiwa huduma ya umeme kupitia Mradi wa REA awamu ya Tatu.

 katika ziara hiyo, Wateja wapatao 96 ambao ni  Wafanyakazi wa Gereza hilo waliweza  kuunganishiwa huduma ya umeme kupitia mradi wa umeme vijijini  awamu ya Tatu. 

Mbali na kuunganishiwa huduma ya umeme Maafisa hao wa Magereza walipatiwa mafunzo juu ya namna ya kupata huduma, matumizi sahihi ya kutumia nishati ya umeme, usalama juu ya umeme, ulinzi wa miundombinu ya umeme na umuhimu wa kutumia umeme ili kuchochea maendeleo Nchi.

Baadhi ya Maafisa wa gereza la Molo wakisikiliza kwa makini elimu na taratibu za kupata umeme kupitia mradi wa umeme vijijini REA 3
              
Mkuu wa Gereza la Mollo ACP J.L  Mwamgunda,Afisa Mahusiano na Huduma kwa Wateja Ndg Lucas C. Kusare na Afisa wa upimaji wakisikiliza maswali kutoka kwa Maofisa wa gereza hilo.

Afisa wa Masoko na Huduma kwa Wateja NMB benki tawi la Sumbawanga akitoa maelezo ya namna ambavyo wateja wa TANESCO wanavyoweza kutumia mfumo wa Benki yao ili kufanya malipo ya huduma mbalimbali za umeme.
Afisa Huduma na Mahusiano kwa Wateja TANESCO Mkoa wa Rukwa akiwafafanulia maofisa wa Gereza la Molo juu ya utaratibu wa kupata huduma ya umeme kupitia mradi wa umeme wa REA 3

Afisa wa Gereza akiulizia utaratibu wa namna ya kupata huduma za umeme kupitia Mpango wa REA 3