December 10, 2016

MAKAMU WA RAIS WA JICA ATEMBELEA KITUO CHA KUPOZA NA KUSAMBAZA UMEME CHA ILALA-MCHIKICHINI JIJINI DAR ES SALAAM

 Mkurugenzi Mtendaji wa Tanesco, Mhandisi Felchesmi Mramba, (kushoto),  akimwelezea jambo Makamu wa Rais wa Shirika la  Serikali ya Japan, linaloshughulikia uratibu wa misada ya maendeleo ya kimataifa, (JICA), Suzuki Noriko,  kuhusu hatua iliyofikiwa na TANESCO katika uboreshaji wa miundombinu ya kupoza na kusambaza umeme alipotembelea kituo cha kupoza na kusambaza umeme cha Ilala-Mchikichini jijini Dar es Salaam, ambapo JICA inashirikana na serikali katika kukiboresha kituo hicho.
Jengo jipya la kituo cha kupoza na kusambaza umeme cha Ilala-Mchikichini jijini Dar es Salaam, ambacho JICA imechangia ujenzi wake.
NA K-VIS BLOG/KHALFAN SAID
Makamu wa Rais wa Shirika la Serikali ya Japan linaloratibu Misada ya Maendeleo laKimataifa (JICA), Bw. Suzuki Noriko ametembelea kituo kipya cha kupoza na kusambaza umeme cha Ilala-Mchikichini kinachoendeshwa na Shirika la Umeme nchini Tanesco.
Ziara hiyo aliifanya Desemba 9, 2016 ambapo Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO Mhandisi Felchesmi Mramba, alimtembeza kujionea hatua mbalimbali zilizofikiwa katika uboreshaji miundombinu ya TANESCO ikiwemo jingo na mitambo.
Ziara hiyo inakuja mwezi mmoja tu baada ya Waziri Mkuu wa Tanzania, Mh. Kassim Majaliwa, kuzindua kituo cha udhibiti na usimamizi wa mifumo ya usambazaji umeme katika jiji la Dar  es salaam kilichoko Mikocheni jijini Dar es Salaam ambapo kituo hicho cha Ilala, ni sehemu ya mradi wa uboreshaji miundombinu ya umeme kwenye jiji hilo.
JICA na mashirika mengine ya kimataifa yanafadhili mradi huo wa uboreshaji umeme jijini ambapo lengo ni kuwapatia wakazi wa jiji umeme ulio bora na wa uhakika zaidi, ambapo utekelezaji wa mradi huu umehusisha ujenzi wa kituo cha kupoza nguvu za umeme chenye ukubwa wa 100MVA (2X50MVA), 132/33KV cha City Centre, ujenzi wa mfumo wa njia ya usafirishaji umeme chini ya ardhi (Underground Transmission Line) na kwa kutumia minara (Overhead Line) ya msongo wa wa kilovolti 132 kutoka kituo cha Ilala hadi kituo cha City Centre umbali wa Kilomita 3.4, vile vile ujenzi wa mfumo wa njia ya usafirishaji umeme chini ya ardhi, (Underground Transmission Line) kutoka kituo cha Makumbusho hadi kituo cha City Centre umbali wa kilomita 6.67.

Mafundi wa TANESCO kwa kushirikiana na wataalamu kutoka Japan, wakimalizia kazi ya kufunga mitambo kwenye kituo hicho cha Ilala


Mhandisi Mramba akizungumza na mwakilishi wa JICA Tanzania Bi.Toshio Nagase


Mhandisi Mramba, akiongoza ujumbe wa JAICA kutembelea kituo hicho.

 Mhandisi Mramba akimshukuru bi Nagase baada ya kutembelea kituo hicho. Katikati ni Meneja Mwandamizi wa TANESCO kanda ya Dar es Salaam na Pwani Mhandisi, Mahende Mgaya.
 Wataalamu wa mitambo ya umeme kutoka Japan, wakijadliana




December 2, 2016

TANESCO YATANGAZA KUWEPO KWA KATIZO LA UMEME KWA BAADHI YA MIKOA ILIYOUNGWA KWENYE GRIDI YA TAIFA

 Mhandisi wa umeme wa Shirika la Umeme nchuini Tanzania TANESCO, akiwa kazini jijini Dar es Salaam

SHIRIKA la Umeme Tanzania (TANESCO) linawatangazia wateja wake wa Mikoa ya Dodoma, Singida, Shinyanga, Tabora, Mwanza,  Geita, Mara, Simiyu na na baadhi ya maeneo ya Mikoa ya  Arusha, Manyara, Kilimanjaro  na Tanga na baadhi ya maeneo ya Mkoa wa Dar es Salaam (Tazara, Mlimani City, Mandela Road, Ubungo na Kimara, Sinza, Mabibo) kuwa yatakosa Umeme siku ya Jumapili DESEMBA 04, 2016 kuanzia saa 02:00 Asubuhi hadi saa 11.00 Jioni.

SABABU: Kuruhusu Mkandarasi anayejenga Njia Kuu ya Kusafirisha Umeme ya Msongo Mkubwa ya Kilovolti 400 maarufu kama (Backbone Transmission Line 400 kV) kutoka Iringa hadi Shinyanga.
SABABU: Kuzimwa kwa njia ya Umeme ya Msongo wa Kilovolti 33 Kituo cha Ubungo Dar es Salaam ilikumruhusu Mkandarasi kufanya matengenezo.

Matengenezo hayo yanalenga kuboresha na kuimarisha hali ya upatikanaji wa Umeme Nchini.
  
Uongozi unaomba radhi kwa usumbufu wowote utakaojitokeza.
Imetolewa na; Ofisi ya Uhusiano
TANESCO Makao Makuu