September 3, 2021

Mkandarasi JNHPP ameshalipwa trilioni 2.7

 


 Mkurugenzi Mtendaji TANESCO, Dkt. Tito Mwinuka amesema Mkandarasi anaetekeleza mradi wa Julius Nyerere (JNHPP) Mw 2115 ameshalipwa jumla ya shilingi trilioni 2.7 kulingana na mpango kazi kati ya shilingi trilioni 6.5 anazotakiwa kulipwa hadi kukamilika kwa mradi.

Dkt. Mwinuka ameyasema hayo leo Ijumaa Septemba 03, 2021 katika ziara ya Sekretarieti ya Baraza la Mawaziri, Wafanyakazi wa Ofisi ya Rais Ikulu na Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora.

Kwa upande wake Karani wa Baraza la Mawaziri, Bw. Nsubili Joshua amesema ameongozana na Maafisa wa Sekritarieti ili kujionea kazi inavyoendelea JNHPP.

Amesema mradi wamekuwa wakiufahamu kwenye makaratasi hivyo wamefika kujionea hali halisi na kuona kinachoendelea.

Ameongeza kuwa wameona mambo makubwa ambayo hawayajatarajia na kutoa pongezi kwa viongozi wakuu Serikalini kwa kuutekeleza mradi huo.

Awali akieleza lengo la ziara hiyo, Katibu Mkuu Ofisi ya Rais Menejimenti ya utumishi wa umma, Bw. Lauren Ndumbaru amesema wamefanya ziara katika mradi na watumishi wa umma wa ngazi zote ili watumishi waweze kuona na kuthamini kazi ambayo Serikali inafanya katika ujenzi wa miradi ya kimkakati.

"Naamini kabisa mradi wa Julius Nyerere ukikamilika utaleta maendeleo makubwa katika Nchi yetu, niombe watumishi wa umma wafanye kazi kwa bili na waendelee kuiunga mkono Serikali ili tuone matokeo mapema" amesema Bw. Ndumbalo

Naibu Katibu Mkuu Nishati, Bw. Kheri Mahimbali amesema Wizara ya Nishati imefarijika kutokana na Ofisi zote mbili kuridhishwa na utekelezaji wa mradi wa Julius Nyerere.

"Tunamshukuru Rais Samia Hassan kwa kuendelea kuuangalia mradi huu kwa jicho la kipekee kabisa, tunapata pesa za kuendeleza mradi kwa wakati na usimamizi mzuri, tutaendelea kuusimamia na kuhakikisha mradi huu unakamilika kwa wakati" amesema Bw. Mahimbila.

 






No comments:

Post a Comment