December 20, 2016

WAHARIRI WATEMBELE MARADI WA UFUAJI UMEME BACKBONE IRINGA-SHINYANGA.



 
Mhandisi Khalid James akizungumza na Wahariri kutoka vyombo mbalimbali vya habari nchini kuhusu mradi wa ‘Backbone’, mradi unaounganisha mikoa ya Iringa, Dodoma, Singida na kuishia Shinyanga katika ofisi za TANESCO mkoani Iringa, jana. (Picha na Mpiga Picha Wetu)
 Na Magreth Subi, Grace Kisyombe

Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO), likishirikiana na vyombo mbalimbali vya habari nchini, limefanya ziara ya kutembelea mradi wa usambaziji wa umeme ‘Backbone’ unaoanzia Iringa na kuishia Shinyanga, mradi unaotarajia kuzinduliwa na Rais wa Jamuhuri ya Muungano Tanzania, Dkt. John Pombe Magufuli, ili kujionea jidtihada za shirika hilo.

Mradi wa backbone unaanzia mkoani Iringa na kupita katika mikoa ya Dodoma, Singida na kuishia Shinyanga, ni mradi mkubwa unaoweka historia toka Tanzania imepata uhuru 1961. Akielezea mradi huo Meneja Mradi, kutoka TANESCO, Mhandisi Khalid Rueben James, alisema mradi huo utawanufaisha Watanzania kwa kupata umeme wa uhakika.

Mhandisi Khalid, alisema “mradi wa backbone utafanya ukarabati wa maeneo ya kupoozea umeme, pamoja na kunufaisha vijiji vilivyoko katika maeneo mradi unapopita.”  Mhandisi Khalid alieleza kuwa wananchi walioko katika vijiji hivyo watapata umeme kwa gharama nafuu kupitia mfuko wa uunganishwaji umeme vijijini (Rural Electrification Fund –REF)

Mhandisi Khalid alisisitiza kuwa vyanzo vingi vya umeme vinapatikana Ukanda wa Nyanda za Juu Kusini, ni pamoja na makaa ya mawe, joto ardhi, upepo  na maji kutoka katika bwawa la mtera. Aidha, alielezea   kwanini waliamua kuanzia mikoa inayo athirika kama Dodoma, Singida, Shinyanga ilikuondokana changamoto ya  kukatika umeme mara kwa mara.

Mhandisi Khalid alisema, mradi huu wa usafirishaji umeme ukikamilika utasaidia kuunganisha gridi ya taifa na gridi nyingine zikiwemo za mataifa jirani kama Kenya, Uganda, Ethiopia na Zambia.

Gharama za mradi wa backbone zimechangiwa na wahisani kutoka nchi mbalimbali ambao ni pamoja na Benki ya Dunia, Benki ya Maendeleo ya Africa (AfDB), Shirika la Maendeleo Japan (JICA), Benki ya Uwekezaji ya Nchi za Ulaya (EIB), Shirika la Kiuchumi la Maendeleo Korea Kusini(EDCF), bila kusahau Serikali ya Jamuhuri ya Muungano Tanzania, Kwa ujumla gharama za  kukamilisha ujenzi wa mradi huu ni dola za  Marekani milioni 473.6

Mradi huu uliosimamiwa na Tanesco ulitekelezwa na wakandarasi ambao ni makampuni matatu ambayo ni KEC International Limimted, JYOTI Structures Ltd zote mbili kutoka India na GSE&C and Hyosung kutoka Korea Kusini. Ujenzi ulianza rasmi mwishoni mwa novemba 2013 na kukamilika kwa wakati ulipangwa kwa asilimia 100, alisema Muhandisi Khalid.

Wahariri kutoka vyombo mbalimbali vya habari nchini wakimsikiliza Mhandisi Khalid James, walipotembelea kituo cha kupoozea umeme cha Tagamenda ambapo ndipo mradi wa Backbone unaanzia, mkoani Iringa jana. Mradi huo unaounganisha mikoa ya Dodoma, Singida na kuishia Shinyanga. (Picha na Mpiga Picha Wetu)

Minara mikubwa ‘Cross Sectional  Tower’ ya umeme yenye urefu wa mita 89.5 na umbali wa kilomita 1.6 kutoka mnara mmoja hadi mwingine katika bwawa la Mtera ni minara mirefu kuliko yote nchini, kama inavyoonekana katika picha. Minara hii ni sehemu ya mradi wa ‘Backbone’ mradi unaounganisha mikoa ya Dodoma, Singida na kuishia Shinyanga. (Picha na Mpiga Picha Wetu)

No comments:

Post a Comment