October 27, 2017

KUKATIKA KWA UMEME NCHI NZIMA: DKT. KALEMANI AWAOMBA RADHI WANANCHI.


WAZIRI wa Nishati, Dkt. Medard Kalemani, (pichani juu), amewaomba radhi Wananchi kufuatia kukatika kwa umeme nchi nzima Oktoba 25 na 26, 2017 kulikosababishwa na hitilafu kwenye mfumo wa Gridi ya Taifa.

Dkt. Kalemani ambaye alikuwa mjini Dodoma akishiriki vikao vya kamati za Bunge, alilazimika kusafiri mapema jana Asubuhi Oktoba 26, 2017 kuja jijini Dar es Salaam ili kufuatilia juhudi za kurekebisha tatizo hilo.

"Ndugu Wananchi hali ilivyotokea sisi kama Shirika la TANESCO na Serikali tunawaomba radhi kwa matatizo yaliyotokea, lakini niseme tu kwamba kuna hatua madhubuti zinazochukuliwa hivi sasa kurekebisha hali hiyo ili Wananchi muendelee kupata umeme wa uhakika." Alisema Dkt. Kalemani katika taarifa yake kwa Wananchi aliyoitoa Makao Makuu ya Wizara jijini Dar es Salaam baada ya ziara yake ya kutembelea kituo cha udhibiti cha Gridi ya Taifa, (GCC), kilichoko Ubungo na kituo cha kufua umeme wa gesi cha Kinyerezi1 jijini Dar es Salaam.

Taarifa za awali zilieleza kuwa kukatika kwa umeme kulisababishwa na "Gridi kuchomoka" Oktoba 25, 2017 majira ya saa 10;08 alfajiri na kurejea saa 12:09 Asubuhi ambapo umeme ulirejea Mikoa yote isipokuwa Zanzibar, ingawa juhudi za mafundi wa TANESCO ziliwezesha umeme kurejea Zanzibar majira ya saa 1 asubuhi.
Hata hivyo tatizo hilo lilirejea tena majira ya saa 12:30 jioni siku hiyo hiyo ya Oktoba 25, 2017, ambapo takriban Mikoa yote iliathirika. Umeme ulirejea tena majira ya saa 3 usiku lakiji ilipofika Oktoba 26, 2017 majira ya saa 12:03 tatizo hilo likajirudia tena na kuathiri takribani Mikoa yote ikiwemo Zanzibar.

"Nimekuja kutoka Dodoma ili kuona nini kimetokea, nini kimesababisha na hatua gani za haraka zinachukuliwa ili kuondoa tatizo hilo, hii ndio hasa dhamira ya safari yangu." Alisema Dkt. Kalemani baada ya kufika kwenye kituo cha udhibiti Gridi ya Taifa, Ubunmgo.

Lakini niwapongeze TANESCO kwa kutoa taarifa mapema kwa Wananchi kuwajulisha kuhusu tatizo hilo, alisema.
Akifafanua zaidi Dkt. Kalemani alisema, chanzo cha tatizo ni pamoja na mfumo wenyewe (GCC) na bado unafanyiwa marekebisho na taratibu zinaendelea, na kule Kinyerezi kuna mashine moja haifanyi kazi nayo inafanyiwa marekebisho ikiwa ni pamoja na Valvu moja iliyoharibika nayo pia inafabnyiwa kazi.

"Gridi ya Taifa imerejea tangu usiku wa Oktoba 25, na umeme unapatikana nchi nzima lakini hata hivyo yapo maeneo machache ambayo hayapati umeme wa kutosha kwa sababu mtambo mmoja wa Ubungo namba mbili wenye jumla ya megawati 129 haujaanza kufanya kazi na nimeelekeza wataalamu wafanye kazi usiku na mchana na wamenihakikishia kufikia saa 5 asubuhi kesho (Oktoka 27), mtambo huo utaanza kufanya kazi na umeme utarejea katika hali yake ya kawaida." Alibainisha.

Dkt. Kalemani akiwa kwenye kituo cha udhibiti wa Gridi ya Taifa (GCC), Ubungo jijini Dar es Salaam
Naibu Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO, anayeshughulikia uzalishaji (Generation), Mhandisi Abdallah Ikwasa, (kushoto), akimpatia maelezo Waziri Dkt. Kalemani alipotembelea mitambo ya kufua umeme ya Kinyerezi 1 jijini Oktoba 26, 2017. Wakzanza kulia ni NJaibu Katibu Mkuu Nishati, Dkt. Juliana Palagyo
Meneja Mwandamizi wa TANESCO, anayeshughulikia uzalishaji, Mhandisi Costa Rubagumya akifafanua jambo.
Meneja wa udhibiti ifumo ya Gridi ya Taifa (Protection), Mhandisi Izahaki Mosha, akimfafanulia Waziri Dkt. Kalemani (kushoto).
Dkt. Kalemani (kushoto), akiwa kwenye chumba cha udhibiti cha Kinyerezi 1 akifafanua jambo.

No comments:

Post a Comment