August 16, 2018

Waziri kalemani awasha rasmi umeme katika Mahakama ya mwanzo ya Somanda

Waziri wa Nishati, Dkt. Medard Kalema akikata utepe.

Mahakama ya mwanzo ya Somanda
Waziri wa Nishati, Dkt. Medard Kalemani amewasha rasmi umeme katika Mahakama ya Mwanzo ya Somanda Wilayani Bariadi Mkoa wa Simiyu kupitia Mradi wa Umeme Vijijini Awamu ya Tatu (REA 111).

Waziri Kalemani amefanya uzinduzi huo jana, Agosti 15, 2018 katika eneo la Mahakama ya Mwanzo ya Somanda mkoani Simiyu akiwa katika ziara yake katika Kanda ya Ziwa.

Waziri Kalemani alieleza kuwa ni faraja kwake kuona taasisi za umma zikiwemo Mahakama zikipata umeme.

“Mahakama nyingi zilikuwa hazina umeme, na hii ni mojawapo ya changamoto ambayo inapekea kesi nyingi mahakama kuchelewa, hivyo Mahakama ya Somanda mtaharakisha kutoa hukumu ya kesi ili kutenda haki kwa wananchi” alisema Waziri Kalemani.

Waziri Kalemani alisema kuwa, kipaumbele cha Serikali ni kupeleka nishati ya umeme katika Taasisi zote za umeme ili kuwafikia wananchi wengi kwa wakati moja.

Akizungumza katika mkutano huo, Waziri Kalemani alisema kuwa sasa mahakama ya Somanda watafanya kazi zao muda wowote na pia wanaweza kuweka vinasa sauti ili kupata ushahidi wa uhakika kutoka kwa mashahidi wao.

Aidha, Waziri Kalemani alikumbusha Mahakama hiyo kulipia bili zao za umeme kwa wakati ili kuepuka kukatiwa umeme na kusababisha usumbufu kwa wananchi.
Pia, Waziri Kalemani aliagiza Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) kuweka Transforma moja katika mahakama hiyo special kwao wao wenyewe ili kuepuka usumbufu wowote utakaojitokeza kama vile kukatika kwa umeme.

“Wekeni Transfoma ya Mahakama hii wao peke yake ili ikitokea umeme umekatika maeneo mengine wao wasipate usumbufu ili wafanye kazi yao kwa ufanisi,”alisema Waziri Kalemani.

Waziri Kalemani pia, alikabizi vifaa cha Umeme Tayari (UMETA) 20 kwa Mahakama hiyo lengo likiwa ni kuhamasisha matumizi ya vifaa hivyo vya UMETA katika Taasisi za umma ambavyo havihitaji gharama kubwa kuviunganisha na vinawasha vyuma viwili hadi vinne.


Waziri wa Nishati, Dkt. Medard Kalemani (wa tatu kulia) akishangilia mara baada ya kukata utepe ikiwa ni ishara ya kuwasha rasmi umeme katika Mahakama hiyo. Wa pili kulia ni Mkuu wa Mkoa wa Simiyu Antony Mktaka na wa tano kulia ni Hakimu wa Mahakama ya Mwanzo David Peter.


Waziri wa Nishati, Dkt. Medard Kalemani( katikati kwa waliokaa) akiwa katika picha ya pamoja mara bada ya kuwasha umeme rasmi katika Mahaka ya Mwanzo ya Somanda wilayani Bariadi. Wengine katika picha ni Wafanyakazi kutoka Serekalini.



No comments:

Post a Comment