Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti wakiongozwa na Mwenyekiti
wa Kamati, George Simbachawene leo wametembelea kiwanda cha kuzalisha
transfoma cha TANELEC kilichoko jijini Arusha ili kukagua masuala
mbalimbali ikiwemo uwezo wa uzalishaji wa transfoma.
Katika ziara hiyo waliambatana na Waziri wa Nishati, Dkt Medard Kalemani
na watendaji mbalimbali kutoka Wizara ya Nishati, Shirika la Umeme
Tanzania ( TANESCO) na Wakala wa Nishati Vijijini (REA).
Baada ya kukagua shughuli za uzalishaji wa transfoma katika Kiwanda
hicho, Wajumbe hao kwa nyakati tofauti waliowapongeza watendaji wa
Kiwanda hicho kwa kuzalisha transfoma nyingi ambazo ni 14,000 kwa mwaka
huku mahitaji ya transfoma kwa mwaka yakiwa ni 10,000.
Aidha Wajumbe hao wamepongeza uamuzi wa Serikali wa mwaka 2017 ambao
ulielekeza kuwa miradi yote ya umeme nchini itumie vifaa vya umeme
vinavyopatikana nchini hali inayopelekea miradi hiyo kufanyika kwa kasi.
Wajumbe hao pia wamemtaka Mkurugenzi Mkuu wa kampuni hiyo kuongeza
uzalishaji na kuwa mbunifu kwa kuangalia pia masoko mengine ya transfoma
na si kulenga miradi ya umeme ya ndani ya nchi pekee.
Awali, Waziri wa Nishati, Dkt Medard Kalemani alisema kuwa, Serikali
ilichukua uamuzi wa kusitisha kuagiza nje vifaa vya umeme
vinavyopatikana nchini ili kuongeza kasi ya utekelezaji wa miradi ya
umeme.
Alitoa mfano kuwa upatikanaji wa transfoma nje ya nchi unaweza kuchukua
hadi miezi 12 wakati transfoma zinazozalishwa ndani ya nchi zinachukua
muda mfupi kufika katika eneo zinapohitajika.
Aidha Waziri wa Nishati alisema kuwa uagizaji wa transfoma nje ya nchi
ni gharama kubwa kwani transfoma moja kutoka nje ya nchi inauzwa kwa
takriban shilingi milioni Tisa wakati zinazozalishwa nchini ni takriban
shilingi milioni 6.5.
Akitoa taarifa ya kiwanda hicho, Mkurugenzi Mkuu wa TANELEC, Zahir Saleh
alisema kuwa kiwanda hicho kilichoanzishwa mwaka 1981 kwa sasa
kinazalisha transfoma kiasi cha 14,000 kwa mwaka.
Alisema kuwa, kiwanda kinazalisha transfoma za uwezo wa kvA 50 hadi kVA
5000 na kufanya matengenezo ya transfoma kutoka nchi mbalimbali za
Afrika kama Rwanda, Burundi na Kenya.
Aliongeza kuwa, uamuzi wa Serikali kuzuia kuagiza vifaa nje ya nchi
umekinufaisha kiwanda hicho kwani kabla ya uamuzi walikuwa wakizalisha
transfoma 7000 kwa mwaka lakini sasa wanazalisha transfoma 14,000.
Kuhusu ajira alisema kuwa, awali waliajiri wafanyakazi 30 lakini kwa
sasa wafanyakazi walioajiriwa ni 70 na kwa mwaka huu wataajiri
wafanyakazi wengine 40.
Vilevile alisema kuwa kutokana na uamuzi huo wa Serikali, Kiwanda
kinafanya kazi kwa faida na wameanza kupeleka gawio serikalini la
takribani shilingi milioni 500 kwa mwaka 2018 na wanategemea kuongeza
kiasi cha gawio hilo kwa miaka inayokuja.