January 7, 2018

Waziri Mkuu: “Umeme ni fedha, Kuwepo kwa Umeme ni Ajira tosha”





Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Kassim M. Majaliwa akiwa katika ziara ya kikazi Mkoani Ruvuma ameweka jiwe la msingi la mradi wa njia ya kusafirisha umeme ya msongo wa kilovolti 220 kutoka Makambako hadi Songea pamoja na ujenzi wa jengo la Ofisi ya TANESCO Mkoani Ruvuma.
Mheshimiwa Majaliwa amesema lengo la ziara hiyo ni kuwatayarisha Wananchi juu ya miradi mbalimbali ya maendeleo inayotekelezwa na Serikali huku akieleza msimamo wa Serikali ni maslahi ya nchi kwanza.

Aliongeza, mkakati wa Serikali ya Awamu ya Tano katika Sekta ya Nishati, ni kuona mtandao wa umeme unaenea pote nchini,  na katika Vijiji ambavyo ni vigumu kufikika kwa miundombinu ya umeme Vijiji hivyo vitatumia umeme wa jua (Solar System).
Ameipongeza Bodi ya Wakurugenzi TANESCO kupitia kwa Mwenyekiti wake Dkt. Alexander Kyaruzi, Menejimenti ya TANESCO pamoja na Wafanyakazi kwa kuunga mkono katika utekelezaji wa Sera za Serikali. 

“Nimpongeze Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi TANESCO Dkt. Alexander Kyaruzi kwa namna Bodi inavyosimamia, hongera sana wana TANESCO kwa kuunga mkono jitihada za Serikali”. Alisema Mhe. Majaliwa.

Aidha, alisema amefarijika sana kwa kuhakikishiwa ujenzi wa njia ya kusafirisha umeme kutoka Makambako hadi Songea kukamilika mwishoni mwa mwezi Agosti na jingo la Ofisi mwezi Machi mwaka huu.

Aliongeza kufika kwa umeme wa gridi kutafungua fursa za kibiashara kwa Wananchi wa maeneo hayo hivyo kutokuwepo malalamiko ya ukosefu wa ajira kwa watu kujiari, “Ndugu zangu Umeme ni fedha, Kuwepo kwa Umeme ni Ajira tosha, hivyo tuwekeze katika biashara ndogo ndogo za kutuingizia kipato”.

Kwa upande wake, Waziri wa Nishati Dkt. Medard Kalemani alisema katika kipindi cha Miaka miwili ya  Uongozi wa Serikali ya Awamu ya Tano kumekuwa na mafanikio katika sekta ya nishati nchini ambapo katika njia za kusafirisha umeme mkubwa zimejengwa mbili ambazo ni mradi wa njia ya kusafirisha umeme wa kilovolti 400 kutoka Iringa hadi Shinyanga na mmradi wa njia ya kusafirisha umeme wa kilovolti 220 kutoka Makambako Mkoani Njombe  hadi Songea Mkoani Ruvuma wenye urefu wa kilometa 250.

Aliongeza kukamilika kwa njia ya kusafirisha umeme ya Makambako hadi Songea kutaipunguzia TANESCO gharama kwa kuacha kutumia mitambo ya kuzalisha umeme kwa kutumia mafuta katika vituo vya Songea, Mbinga Namtumbo na Madaba .







No comments:

Post a Comment