July 30, 2018

Singida yanufaika na Miradi ya Umeme Vijijini (REA)


Afisa Uhusiano na Huduma kwa Wateja Mkoa wa Singida Witness Msumba akiwaelewesha Wananchi wa Kijiji cha Marya juu ya kifaa cha UMETA ambacho ni mbadala wa "Wiring" ndani kwenye nyumba ndogo.


Na Grace Kisyombe - Singida

Shirika la umeme Tanzania (TANESCO)  limeendelea na utoaji elimu kwa umma kuhusu  miradi ya umeme vijijini,
Akizungumzia miradi inayoendelea mkoani Singida Mhandisi Abrahmani Nyenye  ambaye ni Meneja wa TANESCO   Mkoa  wa Singida amesema, "Mkoa wa Singida una jumla ya Wateja 34, 185   ujio wa miradi ya umeme vijijini itaongeza wateja 8648 itakapo kamilika" Ambapo aliitaja miradi iliyopo ni Mradi wa uunganishaji umeme vijijini kupitia ufadhili wa Mradi wa njia ya usafirishaji umeme ya 400kV utokao Iringa hadi shinyanga (BTIP )ambao utawanufaisha wanavijiji walio pitiwa na njia hiyo ya umeme ambapo kwa mkoa wa Singida ni vijiji 39 vitanufaika na mradi huu wa BTIP .

Mradi wa pili ni ule wa REA awamu ya Pili  ambao ulipaswa uwe umekamilika lakini kwa changamoto mbali mbali mradi huu bado unaendelea katika baadhi ya vijiji vya Mkoa wa Singida ,

Mradi wa tatu ni ule wa REA awamu ya Tatu ambao umeanza mnamo mwezi wa tano na utakuwa na awamu tatu zinazo tarajiwa kukamilika mnamo mwaka 2021. Akiendelea kuzungumzia miradi hii Mhandisi Nyenye alisema hadi kukamilika kwa miradi yote mitatu Jumla ya vijiji 156 vitakuwa vimepatiwa umeme.

Akihamasisha uwekezaji mhandisi Nyenye alisema Kuna maeneo ya uwekezaji kama eneo la uchimbaji dhahabu la Sekenke tayari limesha patiwa umeme kwa wawekezaji wawili , na kwa kupitia miradi hii wawekezaji ( wachimbaji wadogowadogo ) wa dhahabu pia watapatiwa huduma ya umeme kuanzia vitalu vya Sekenke 1 hadi Sekenke 5 wachimbaji wote watapatiwa umeme.
Pamoja na kuhamasisha uwekezaji Mhandisi Nyeye aliwaasa wanavijiji kulinda miundombinu ya umeme kwani Serikali imewekeza fedha nyingi katika miradi hii hivyo ni vema wanachi wakalinda miundo mbinu hiyo.

 Akitolea mfano eneo la Sekenke ambapo baadhi ya wananchi walianzisha machimbo katika eneo zilipo nguzo za umeme mkubwa wa 400kV , Mhandisi Nyenye alionya kuhusu kuto kufanya shughuli zozote za kibinadamu  katika njia hizo za umeme kwani ni hatari kwa maisha yao pamoja na hasara kwa Serikali kwani endapo itatokea nguzo hizo zikaanguka .

Naye bi Adelina Lyakurwa ambaye ni afisa Masoko kutoka TANESCO makao makuu, aliwahamasisha wananchi kuhusu kuchangamkia fursa hii ambapo kila mwananchi aliye katika miradi hii yote mitatu afuate taratibu za kuunganishiwa umeme kwani katika muda wa mradi mteja atalipia tshs 27,000 tu ili apatiwe huduma. Gharama ambayo ni kodi ya ongezeko la.thamani pekee.

Meneja wa TANESCO Mkoa wa Singida Mhandisi Abrahaman M.A Nyenye akitoa taarifa ya utekelezaji Miradi ya Umeme Mkoani kwake.





No comments:

Post a Comment