March 19, 2012

TANESCO yatoa ufafanuzi - kukatika katika Umeme






Mkurugenzi wa Tanesco Tanzania, Mhandisi. William Mhando ameongea na waandishi wa habari kuelezea hali ya umemeilivyo kwa sasa nchini pia kutoa  ufafanuzi wa tatizo la umeme lililojitokeza katika maeneo tofauti ya jiji la Dar es Salaama.
Ukarabati ukiendelea jijini Dar es Salaam.


Mhandisi Mhando alisema, kukatika mara kwa mara kwa umeme nchini hakutokani na kuwepo kwa mgawo, bali kunasababishwa na kuzidiwa kwa mifumo ya umeme iliyopo na hivyo kushindwa kuhimili kiasi cha umeme unaopita katika mifumo hiyo kutokana na uchakavu wake.
Mhando alisema uchakavu huo wa mifumo ya umeme umetokana na ukweli kwamba shirika hilo lilikaa zaidi ya miaka kumi likiwa katika hati hati ya kubinafsishwa chini ya serĂ¡ ya ubinafsishaji wa mashirika ya umma, hali iliyosababisha mifumo hiyo kutokufanyiwa matengenezo katika kipindi chote hicho.
“Lakini kama haitoshi baadae Shirika lilikabidhiwa  kwa kampuni ya Net Group kutoka Afrika Kusini, ambao waliendesha shirika kwa miaka sita  wakikusanya pesa bila kufanya matengenezo ya mifumo ya umeme kwa kipindi hicho chote, hakukuwa na ajira mpya na wala hakukuwa na mafunzo kwa wafanyakazi wetu”.
Hata hivyo , alisema baada ya mamuzi ya kutolibinafsisha shirika, walianza kuifanyia matengenezo miundombinu hiyo na kwamba wanaendelea kuifanyia ukarabati kwa kutumia fedha kutoka vyanzo vyake na kutoka kwa wahisani.
Mhandisi Mhando alisema, pamoja na Shirika kutenga zaidi ya asilimia 12 kila mwezi ya mapato yake kwa ajili ya ukarabati wa miundombinu pia wamepatiwa dola za Kimarekani milioni 85 kutoka kwa marafiki wa maendeleo ambazo zinatumika kuboresha mifumo ya umeme katika jiji la Dar es Salaam, Arusha na Kilimanjaro na dola milioni 50 kutoka Benki ya Maendeleo ya Afrika (ADB) kwa ajili ya vituo vilivyoko Dar es Salaam, Shinyanga na Mwanza na Euro millioni 25 kwa ajili ya kuboresha mifumo ya umeme iliyoko katikati ya jiji la Dar es Salaam.
Akielezea tatizo la hujuma ya miundombunu ya shirika kama sababu kubwa inayosababisha kukatika kwa umeme, Mhandisi Mhando, alisema;
“Uhujumu katika miundombinu yetu vilevile umekuwa ukisababisha tatizo la kukatika umeme mara kwa mara katika maeneo mbalimbali nchini. Kwa mfano katika maeneo yanayohudumiwa na TANESCO Kinondoni, kati ya Disemba mwaka jana hadi Machi mwaka huu, jumla ya transfoma 21 zenye thamani ya shilingi milioni 400 zilihujumiwa”.
Kuhusu mkopo wa bilioni  408 kutoka kutoka benki ya Citybank, Mhandisi Mhando alisema, mkopo huo upo katika hatua za mwisho na serikali itatoa thamana wiki hii ijayo (wiki hii) hivyo utasaidia katika kuboresha miundombinu na kuongeza uzalishaji wa umeme.
Kwa mujibu wa taarifa hiyo, kuhusu mpango wa dharura uliowasilishwa bungeni mwaka jana kwenye bunge la bajeti wa kuzalisha megawati 572, hadi sasa jumla ya megawati 342 zimeshaingizwa kwenye gridi ya taifa.

Hadi kufikia Disemba 18, 2012 jumla ya uzalishaji wa umeme kwa vituo vyote nchini  ulikuwa ni megawati 718 ambapo mahitaji ya kawaida ya nchi nzima ni kati ya megawati 600 na 829. 





 Transfoma hizi zote zimeharibika ama kulipuka 
baada ya kuibiwa mafuta kwa mkoa wa Kinondoni Kaskazini pekee, 
ni sehemu ya zile 21, alizozielezea Mkurugenzi.

2 comments:

  1. Mbona hajaelezea tatizo la upatikaji wa mita?

    ReplyDelete
  2. Tanesco mnafanya kazi kubwa sana katika nchi hii hilo linafahamika japokuwa baadhi ya watanzania watapinga hilo. kwa nini? watanzania huwa hatupendi kukubali ukweli hasa penye tatizo ambalo lipo wazi.lakini nikirudi upande wa shirika kwa ujumla mapungufu yapo basi myatumie mapungufu hayo kama changa moto kwenu.mara nyingi sisi wateja huwatunafahamu matatizo mbalimbali yanayotokea lakini TAARIFA ni kitu muhimu sana kwetu sisi wateja.Nimpongeze tu kijana mmoja huwa tunamwona maeneo mbalimbali kama vile G/mboto,Vingunguti akifanya matangazo ya kuhamasisha wateja kuomba umeme,mapambano zidi ya vishoka,njia za kununua luku,misamaha ya riba na matatizo mbalimbali ya umeme yanapojitokeza na nk.,pia
    nilimwona akifanya matangazo ya kuwaondoa wamachinga na aina mbalimbali ya matangazo yanayohusu shirika la umeme Tanesco.tunampongeza sana lakini mpeni tangazo linalo husu upatikanaji wa mita na sisi tunaotumia mita za kuchomeka kadi wapi tununue? hatujaona akitueleza wapi tununue umeme.lakini tunasikitika kuona gari analotumia kufanya kazi hiyo halipo sahii ukizingatia na shirika lilivyo kwani halipo kimatangazo tungetegemea kuona gari linabandikwa matangazo mbalimbali, msema matangazo anayunifomu.hakuna kampuni inayofanya vizuri bila matangazo kwani hali ya sasa ni ya ushindani zaidi angalieni makapuni ya simu, viwanda vya sabuni na mengine mengi sasa hivi hata wamachinga wanafanya promotion hamkeni Tanesco na pia mlifanye shirika kuwa la kibiashara na sio la kisiasa kama linavyoonekana.NAAMINI KUWA UWEZO MNAO, NIA MNAYO BADILIKENI.tAARIFA NIKITU MUHIMU SANA.WATU WA MITA RUSHWA IMEZIDI KWA MAFUNDI WENU MPAKA CUSTOMER CARE. CASH OFISI ZENU A/C HAKUNA WAKATI BILI ZINALIPWA NAKO TATIZO NI NINI?

    ReplyDelete